KIDATO CHA NNE
MADA YA KWANZA: KUONGEZA MSAMIATI WA
KISWAHILI
Uundaji wa Maneno
Lugha hukua na kubadilika kila
wakati kulingana na maendeleo ya jamii. Kigezo kimojawapo cha kukua na
kubadilika kwa lugha ni kuongezeka kwa msamiati. Ili msamiati uongezeke katika
lugha sharti maneno mapya yaundwe.
Njia za Uundaji Maneno
Uundaji wa Msamiati hutokea kwa njia
mbalimbali zifuatazo:
- Kubadili mpangilio wa herufi.
- Kuambatanisha maneno.
- Kutohoa maneno ya lugha
nyingine.
- Uambishaji wa maneno.
- Kufanikisha sauti, umbo, mlio
na sura.
Kuunda msamiati kwa kubadili mpangilio wa herufi
Neno hujengwa kwa vitamkwa au
herufi. Neno jipya lenye maana tofauti huweza kuundwa kwa kubadili mpangilio wa
neno lingine
Mfano
- Neno lima, lina herufi l, i, m,
a, herufi hizi huweza kujenga maneno kama mali, kumi,imla, mila.
- Neno tua lina herufi t, u, a,
herufi hizi zina weza kujenga maneno kama:- tatu, tua, viatu, tatua.
Njia ya kuambatanisha maneno
Kuna njia tatu za kuambatanisha
meneno
Njia ya kurudufisha au kukariri neno
Mfano; barabara, sawasawa, polepole, katikati,
vilevile.
Njia ya uundaji wa Msamiati kwa
kuunganisha maneno mawili tofauti
Nomino na Nomino
- Punda + mlia unapata Pundamilia
- Bibi + Shamba unapata Bibishamba
- Afisa + Elimu unapata
Afisaelimu
- Mwana + Siasa unapata
Mwanasiasa
- Bata + maji unapata Batamaji
Kuunganisha kitenzi na Nomino/Jina
- Changa + moto changamoto
- Chemsha + bongo chemshabongo
- Piga + mbizi pigambizi
- Zima + moto zimamoto
Kuunganisha maneno mawili na
kudondosha baadhi ya herufi
Mfano
- Baraza la Kiswahili Tanzania
BAKITA
- Mzaliwa wa mahali Fulani MZAWA
- Chama cha Mapinduzi CCM
- Nyamamfu NYAMAFU
Kutohoa maneno kutoka lugha nyingine
Kila lugha na tabia ya kuchukua
maneno lugha nyingine ili kukidhi mahitaji ya Msamiati. Maneno kutoka lugha
nyingine yanapoteuliwa hubadilishwa kimatamshiili ya fuate kanuniza Kiswahili.
Maneno yanayotoholewa kutoka lugha
nyingine husanifishwa na asasi za lugha ya Kiswahili ndipo ya ruhusiwe kutumiwa
rasmi.
Mfano
Neno la Kiswahili
|
Lugha ya Mwanzo
|
Neno Lililotoholewa
|
Kijerumani
|
Schule
|
|
Salama
|
Kiarabu
|
Salaam
|
Duka
|
Kihindi
|
Dukan
|
Karoti
|
Kiingereza
|
Carrot
|
Shati
|
Kiingereza
|
Shirt
|
Picha
|
Kiingereza
|
Picture
|
Papai
|
Kihispania
|
Papaya
|
Meza
|
Kireno
|
Mezi
|
Shukrani
|
Kiarabu
|
Shukran
|
Ngeli
|
Kihaya
|
Engeli
|
Ikulu
|
Kinyamwezi
|
Ikulu
|
Ng'atuka
|
Kizanaki
|
Ng'atuka
|
Ndafu
|
Kichaga
|
Ndafu
|
Namba
|
Kuunda maneno kwa njia ya uambishaji
wa maneno
Hii ni njia ya kubandika viambishi
awali na tamati kwe nyekiini. Ujenzi wa maneno hutokana na mzizi mmoja kuonesha
maana tofauti ingawa maana zina husiana.
Mfano mzizi: -lim-.Tukipachika
viambishi awali na tamati tunapata maneno kama lima, analima, walilima, kilimo,
limiana,halitalimwa na ukulima.
Kufananisha sauti, sura au tabia
Example 4
Mfano
- Kengele - utokana na sauti ya
kengele inapo pigwa
- Pikipiki - hutokana na
muungurumo wa pikipiki
- Ndizi mkono wa tembo – Ndizi
inayo fananishwa na mkono wa mnyama tembo
- Chubwi - Jiwe au chura
atumbukiapo katika kina cha maji.
Mazingira yanayoelezea Kuhitaji
Maneno Mapya
Mabadiliko mengi yanatokea kila siku
katika nyanja mbalimbali za kimaisha-mabadiliko ya kiuchumi, kisiasa, kisayansi
na kiteknolojia. Katika mazingira kama haya, watu watahitaji kuwasiliana, lugha
itahitaji kuunda maneno ili kuwasilisha dhana mpya zilizoibuka. Kwa mfano,
maneno kama vile nywila, kisakuzi, udukuzi, puku, talakirishi n.k yameundwa ili
kuwasilisha dhana za kiteknoljia kwa Kiswahili.
Undaji wa Maneno katika Miktadha
mbalimbali
Mabadiliko ya kimaendeleo yanafanya
lugha ihitaji maneno ya kuyafikisha na kutumiwa na jamii. Ili kukidhi mahitaji
hayo, maneno mapya yanazuka. Maneno hayo yanaweza kuwa katika fani mbalimbali,
kama vile sayansi na teknolojia, siasa, utamaduni na uchumi kulingana na mkondo
wa maendeleo. Mfano wa msamiati ni kama vile fedha, ushuru, kumpyuta, ukoloni,
hospitali, suruali n.k
MADA YA PILI: UENEAJI WA KISWAHILI ENZI
ZA WAINGEREZA NA BAADA YA UHURU
Ukuaji na ueneaji wa
Kiswahili katika enzi ya Waingereza
Mambo waliyochangia Waingereza
katika Ukuaji wa Kiswahili nchini Tanzania
Waingereza walipochukua koloni la
Tanganyika kutoka kwa Wajerumani walikuta Kiswahili kimeimarika na kinatumika
katika maeneo mengi ya nchi. Kwa kuwa nao walihitaji kutawala hawakupuuzia
matumizi ya Kiswahili katika utawala wao japo hawakutumia Kiswahili kwa lengo
la kukikuza lakini walijikuta wanakieneza na kukikuza bila ya wao kukusudia.
Waingereza walitumia Kiswahili kama
nyenzo ya kusaidia shughuli zao za kiutawala. Hata hivyo kuna mambo waliyofanya
waingereza yaliyosaidia kukua na kuenea kwa Kiswahili, mambo hayo ni kama
yafuatayo:
Shuguli za kiuchumi
Shuguli za kiuchumi wakati wa
Waingereza zilihusisha kilimo na biashara. Kwa upande wa klimo, Waingereza
waliendesha kilimo cha mazao mbalimbali, na walitumia mfumo wa kuajiri vibarua
kutoka sehemu mbalimbali za nchi. Vibarua hao walijulikana kwa jina la manamba.
Katika mkusanyiko wa vibarua hawa
waliokuwa na usuli wa makabila tofautitofauti, lugha pekee iliyoweza
kuwaunganisha ni Kiswahili ikizingatiwa kwamba Kiswahili kiliteuliwa kuwa lugha
rasimi katika mawasiliano ya kiutawala. Walilazimika kuzungumza Kiswahili kwani
bila hivyo mawasiliano yasingeweza kufanyika kwa urahisi.
Hata hivyo kupitia shuguli za kilimo
maneno mapya ya Kiswahili yaliweza kuzaliwa, kwa mfano: yadi, belo, belingi,
bani, mtama n.k, kwa hiyo kupitia shughuli hizi Kiswahili kilizidi kukua.
Shuguli za kiutamaduni
Shughuli hizi ni kama vile uigizaji
wa tamthiliya za kigeni, uchezaji wa mziki wa kigeni hususani twisti.
Tamthiliya za kigeni zilikuwa zikiigizwa majukwaani kwa lugha ya Kiswahili na
hivyo ikasaidia kukua kwa msamiati wa Kiswahili.
Shughuli za kidini
Wakati wa utawala wa mwingereza pia
kuliambatana na ujio wa wamishonari waliokuwa na lengo la kueneza dini ya
kikristo.
Katika harakati hizi walitumia lugha
ya Kiswahili ili kufanikisha malengo yao ikizingatiwa kwamba Kiswahili kilikuwa
kimeshaenea vya kutosha wakati wa utawala wa Mjerumani, kwa hiyo wamishonari wa
Kiingereza waliendelea kukiimarisha zaidi.
Pia shughuli za kidini zilipelekea
kutafsiriwa kwa vitabu mbalimbali vya kidini kama vile Biblia na vitabu
vingine. Tafsiri ya vitabu hivi ilikuwa ni kutoka katika lugha ya kiingereza
kwenda katika lugha ya Kiswahili. kwa kufanya hivi Kiswahili kiliweza kuingiza
msamiati mwingi sana na hivyo kukuza lugha ya Kiswahili.
Wamishonari walilazimika kujifunza
Kiswahili hukohuko kwao ili wanapokuja huku Afrika Mashariki wasipate tabu ya
kujifunza Kiswahili. Kwa sababu hii wamishonari waliokuwa wamekwishajifunza
lugha ya Kiswahili walitunga kamusi za Kiswahili – Kiingereza ili kuwasaidia
wenzao pia kujifunza Kiswahili; kwa njia hii waliweza kukikuza Kiswahili.
Shughuli za kisiasa
Shughuli za kisiasa hasa katika
uanzishwaji wa vyombo mbalimbali vya kiutawala, jeshi, polisi, mahakama, boma
n.k. Kufuatia uanzishwaji wa vyombo hivi msamiati mwingi wa Kiswahili uliweza
kuzuka na hivyo kukuza Kiswahili.
Shughuli za kiutawala
Makampuni ya uchapishaji
yalianzishwa (East African literature Bureau), na kamati ya lugha iliundwa
(Interterritorian language committee). Hatua hii iliimarisha matumizi ya lugha
ya Kiswahili hali iliyosaidia kukua kwa lugha ya Kiswahili.
Shuguli za ujenzi wa reli na
barabara
Shughuli hizi pia zilisaidia kuibuka
kwa msamiati mpya kama vile, reli, stesheni, tiketi n.k.
Usanifishaji wa Kiswahili
Usanifishaji wa lugha ya Kiswahili
pia lilikua ni jambo jingine muhimu sana lililosaidia kukua kwa msamiati wa Kiswahili.
Lengo la usanifishaji wa Kiswahili lilikuwa ni kuleta ulinganifu wa matumizi ya
lugha ya Kiswahili katika ukanda wa Afrika Mashariki.
UENEAJI WA KISWAHILI
Ukuaji na Ueneaji ni maneno mawili
yenye maana zinazokaribiana lakini zinazotofautiana. Ukuaji humaanisha ongezeko
la msamiati katika lugha na ueneaji ni uongezekaji wa matumizi ya lugha kieneo.
Kwa hiyo hapa tutaangalia yale mambo yaliyosababisha Kiswahili kitumike katika
eneo kubwa. Mambo hayo ni haya yafuatayo:
Vyombo vya habari
Vyombo vya habari vilivyokuwepo kwa
wakati huo ni redio, magazeti na majarida mbalimbali. Kwa upande wa redio
kulikuwepo na redio Tanganyika iliyoanza kurusha matangazo yake kwa kutumia
lugha ya Kiswahili. Na magazeti yaliyokuwa yakichapishwa wakati huo ni pamoja
na: Mambo leo, Sauti ya Pwani, Kiongozi na Habari za leo. Magazeti haya yote
yalikuwa yakichapishwa kwa lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo kwa kutumia vyombo vya
habari (redio na magazeti) kiswahili kiliweza kuenea.
Kilimo
Kupitia kilimo watu waliweza
kukutana pamoja, watu wa makabila tofautitofauti. Kwa hiyo katika kipindi chote
walichokaa kwenye makambi ya mashambani waliweza kujifunza Kiswahili na
walipomaliza muda wao walirudi nyumbani wakiwa wamejifunza lugha mpya na hivo
kwa njia hii waliweza kuieneza lugha ya Kiswahili.
Muundo wa jeshi la kikoloni (KAR)
Jeshi la KAR liliundwa na watu
kutoka makabila mablimbali, na lugha iliyokuwa ikitumika jeshini ni Kiswahili,
askari hawa walisaidia kueneza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kwani
kila walipokwenda walikuwa wakizungumza Kiswahili.
Mfumo wa elimu
Chini ya utawala wa Waingereza
Kiswahili kilitumika katika masomo yote kwa ngazi ya shule ya msingi, na pia
kilitumika kama somo kwa ngazi ya shule za sekondari. Kwa hiyo hii pia
ilichangia kuenea kwa lugha ya Kiswahili
Harakati za kudai uhuru
Chama cha TANU kilianzisha harakati
za kudai uhuru, harakati hizo ziliendeshwa kwa lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo
kupitia harakati hizo Kiswahili kiliweza kuenea kwa kiwango kikubwa.
Tathimini ya maendeleo ya Kiswahili
wakati wa Waingereza
Licha ya maendeleo ya lugha ya
Kiswahili katika utawala wa Waingereza, pia kulikuwa na changamoto
zilizoikabili lugha ya Kiswahili katika kupiga hatua ya maendeleo. Changamoto
hizo ni kama zifuatazo:
Kutofundishwa kwa Kiswahili shule
zote nchini
Wakati wa utawala wa Waingereza
Kiswahili kilifundishwa katika shule za watoto wa kiafrika tu, wakati katika
shule za watoto wa kizungu Kiswahili hakikufundishwa. Kwa hiyo suala hili
lilifanya Kiswahili kipewe msukumo mdogo sana na hivyo kuhafifisha ukuaji wake.
Kutotumika kwa Kiswahili kama lugha
ya kufundishia
Lugha ya Kiswahili ilitumika
kufundishia katika shule za msingi pekee ilihali lugha ya kiingereza ilitumika
kuanzia shule za sekondari hadi elimu ya juu. Hali hii ilisababisha watu
kujitahidi sana kujifunza kiingereza; kwa kuzungumza kiingereza ilikuwa na
ishara kwamba wewe ni msomi, na hivyo kutokana na hali hii Kiswahili kilendelea
kukua polepole sana.
Kukosekana kwa vyombo vya kizalendo
vya kukuza Kiswahili
Vyombo vilivyokuwa vinahusika na
masuala ya ukuzaji wa Kiswahili wakati wa ukoloni vilikuwa vimeanzishwa na
wakoloni wenyewe, kwa mfano Kamati ya Lugha ya Afrika Mashariki
(Inter-Territorial Swahili Language commitee) na Shirika la maandiko la Afrika
Mashariki (East African Literature Bureau). Katika hali kama hii ukuzaji wa
Kiswahili ulikosa msukumo mkubwa wa kizalendo.
Kasumba ya kuthamini Kiingereza
Wananchi walikuwa na kasumba kwamba
mtu anayezungumza Kiingereza alichukuliwa kuwa ni mtu mwenye maendeleo na
msomi, kwa hiyo hali hii ikapelekea watu kutothamini Kiswahili na hivyo
Kiswahili kudharaulika.
Ukuaji na Ueneaji wa
Kiswahili baada ya Uhuru
Shughuli mbalimbali zinazowezesha
Kukua na Kuenea kwa Kiswahili nchini
Baada ya uhuru kuna harakati
mbalimbali zilizochukuliwa na serikali ya Tanzania katika kukiendeleza na
kukikuza kiswahili. Harakati hizo ni pamoja na kupendekezwa kuwa lugha rasmi
1962. Mkwaka 1964 kiswahili kilipendekezwa kuwa lugha ya taifa na kuwa
kitatumika katika shughuli zote za kiserikali na kitaifa mfano katika elimu
hususani elimu ya msingi.
Kuundwa kwa Chombo cha usanifishaji
ambacho kilikuwa na kazi ya kuhimiza maendeleo ya kiswahili, kutayarisha kamusi
na vitabu mbalimbali vya sarufi na fasihi ya lugha ya kiswahili na kuandaa
wataalamu watakaoshughulikia usanifishaji wa Kiswahili
Pia baada ya uhuru kulianzishwa
Taasisi mbalimbali zitakazoshughulikia lugha ya kiswahili. Mfano:- BAKITA,
TUKI, TUMI, UKUTA, UWAVITA, Idara ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaamu.
Baada ya uhuru nchini Tanzania
kiswahili kilienea kwa kasi kubwa sana. Kuna sababu mbalimbali ambazo
zilichangia kukua na kuenea kwa kiswahili hapa nchini. Baadhi ya sababu hizo ni
pamoja na kuteuliwa kwa kiswahili kuwa lugha ya Taifa, Kiswahili kitumike
katika Elimu, mfano kuwa lugha ya kufundishia katika shule za msingi. Kuundwa
kwa vyombo mbalimbali vya kukuza na kuneza kiswahili, Kiswahili kuwa Lugha
rasmi na lugha ya Taifa, shughuli mbalimbali za kidini, shughuli za kisiasa na
kiutawala na shughuli za kiutamaduni na uchapishaji wa vitabu na majarida
mbalimbali.
Kiswahili kuwa lugha ya taifa
Baada ya uhuru mwaka 1962 kamati
iliundwa ili kuangalia uwezekano wa kutumia kiswahili katika shughuli zote rasmi,
mfano bungeni na shughuli zote za kiofisi. Pia kiswahili kiliteuliwa kuwa lugha
ya taifa 1964 ambapo katika shughuli zote za kitaifa zitaendeshwa kwa kutumia
lugha ya kiswahili. Hivyo kiswahili kilihimizwa kutumika katika mawasiliano
yote hasa katika shughuli za umma na Wizara zote, Serikali na Bunge, kiswahili
kiliendelea kupanda hadhi zaidi wakati wa Azimio la Arusha la mwaka 1967 kwani
azimio hilo lilitungwa na kuandikwa kwa lugha ya kiswahili.
Kuundwa kwa vyombo vya ukuzaji na
uenezaji wa Kiswahili
Tanzania baada ya uhuru ilifanya
jitihada za kuunda vyombo mbalimbali vya kukuza na kueneza Kiswahili katika
nyanja mbalimbali mfano wa vyombo hivyo ni UWAVITA BAKITA, TUKI, Taasisi ya
Elimu, TAKILUKI na Chama cha Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam.
Kutumika katika elimu
Kiswahili licha ya kutumika katika
shughuli mbalimbali za kiserikali, kilipendekezwa kutumika katika shule za
Msingi na kufundishwa katika elimu ya sekondari kama somo na katika vyuo vikuu
wanatoa shahada mbalimbali za lugha ya kiswahili. Pia katika Elimu ya watu
wazima ambao hawakujua kusoma na kuandika. Watu hawa walijifunza masomo
mbalimbali kwa lugha ya kiswahili na kuwafanya watu wengi kujua kusoma,
kuandika na kuzungumza lugha ya kiswahili fasaha. Kampeni hii ilikuwa kwa nchi
nzima ambapo walijifunza elimu ya Afya, Siasa, Kiswahili, Kilimo na ufundi kwa
lugha ya Kiswahili na kuwafanya watu wengi kuzungumza kiswahili sanifu.
Vyombo vya habari
Tangu uhuru ulipopatikana kuna
vyombo mbalimbali vya habari vilivyoanzishwa. Vyombo hivi hutumika kueneza
kiswahili kwa kiasi kikubwa na hufikiwa na watu wengi licha ya kuwepo kwa
changamoto za kiuchumi. Vyombo hivyo ni magazeti na majarida mbalimbali ambayo
huandikwa kwa lugha ya kiswahili lakini kuna redio na runinga ambazo matangazo
yake hutangazwa kwa lugha ya kiswahili. Hivyo kukifanya kiswahili kuenea kote
ndani na nje ya nchi.
Biashara
Shughuli za kibiashara nchini
husaidia kuenea na kukua kwa kiswahili kutokana na kuwepo kwa makabila tofauti
tofauti ambapo wafanyabiashara huweza kuunganishwa kwa lugha ya kiswahili.
Hivyo kiswahili hudumishwa na kutumika katika biashara hizo.
Shughuli za siasa na utawala
Tangu wakati wa harakati za
kupigania uhuru kiswahili kimetumika kama nyenzo muhimu kuwaunganisha wananchi.
Shughuli za kisiasa zimetumia lugha hii katika kujiimarisha; mfano wakati wa
chama kimoja, Azimio la Arusha na Mfumo wa vyama vingi Kiswahili kimetumika
kama njia kuu ya mawasiliano. Pia katika utawala chama kinachotawala kimekuwa
na harakati za kukiendeleza kiswahilli katika nyanja zote. Ambapo kiswahili
kimekuwa kikitumika katika shughuli zote za kiutawala. Hivyo shughuli za
kisiasa na kiutawala zimechangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza, kukieneza na
kukiendeleza kiswahili.
Uandishi na uchapishaji wa vitabu
Kuibuka kwa waandishi wa vitabu
mbalimbali vya kiswahili vya sarufi na fasihi ambavyo vilichambua kwa kina
mambo mabalimbali yahusuyo lugha ya kiswahili na utamaduni wake, mfano :- F
Nkwera, Shabani Robart, Mathias Mnyapala na Shaffi Adam Shaffi. Waandishi
wengine chipukizi walijitokeza na wanaendelea kujitokeza katika tasnia hii ya
uandishi wa vitabu.
Shughuli za kiutamaduni
Shughuli za kiutamaduni zimechangia
kueneza kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili. Shughuli hizo ni pamoja na
harusi, misiba, matanga na sherehe mbalimbali za kijamii ambazo zimesaidia
kukiendeleza Kiswahili kwa kuwa huwakutanisha watu tofautitofauti katika
shughuli hizo, ambapo huwalazimu kutumia lugha ya kiswahili katika mawasiliano
na kufanya kiswahili kuendelea. Pia katika Sherehe mbalimbali vikundi vya sanaa
na muziki vinavyotumia lugha ya kiswahili kutumbuiza. Vikundi vingine huandaa
nyimbo zao kwa ajili ya kukieneza Kiswahili.
Vyombo vya Ukuzaji na Uenezaji wa
Lugha ya Kiswahili
Tangu Tanzania ipate uhuru hadi sasa
kuna vyombo kadha wa kadha vilivyoanzishwa kwa ajili ya kukuza na kueneza
Kiswahili baadhi ya vyombo hivyo ni hivi vifuatavyo:
BAKITA
Hii ni taasisi ya serikali
iliyoundwa kwa sheria ya Bunge Na.27 ya mwaka 1967 kwa madhumuni ya kukuza
Kiswahili. Kutokana na sheria hii Baraza ndilo mratibu wa kusimamia asasi zote
na mawakala wote wanaokuza Kiswahili katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
BAKITA imekuwa na mchango mkubwa
sana katika ukuzaji na uenezaji wa lugha ya Kiswahili kupitia majukumu yake.
Majukumu ya Baraza kama yalivyofafanuliwa katika sheria hiyo ni haya yfuatayo:
- Kuratibu na kusimamia maendeleo
na matumizi ya Kiswahili nchini kote.
Katika kufanya hivi Baraza lina jukumu la kuhakikisha Kiswahili
kinaendelea na kuhakikisha kuwa matumizi ya Kiswahili yanakuwa sahihi.
- Kushirikiana na vyombo vingine
nchini vinavyojihusisha na maendeleo ya Kiswahili na kuratibu shughuli zao. Vyama vya Kiswahili kama vile CHAKAMA, CHAWAKAMA vina
mchango mkubwa wa kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili kwa kushirikiana na
BAKITA. Ushirikiano wa BAKITA na vyama hivi waweza kuwa ni wa kuto
ushauri, au msaada wa kifedha, kwa mfano BAKITA imekuwa ikiwasaidia
CHAWAKAMA pale wanapokuwa wanataka kufanya makongamano nap engine
wanahitaji msaada wa kifedha, kwa hiyo BAKITA imekuwa ikiwasaidia kifedha.
- Kuhimiza matumizi ya Kiswahili
katika shughuli rasmi na za kawaida.
BAKITA imekuwa ikiandaa vipindi mbalimbli redioni ili kuhimiza matumizi
sahihi ya lugha ya Kiswahili.
- Kushirikiana na mamlaka
zinazohusika kuthibitisha tafsiri sanifu za istilahi. Katiaka uundaji wa istilahi, BAKITA imekuwa
ikichapisha vitabu mbalimbali ikionesha istilahi sanifu zilizoingizwa
katika lugha ya Kiswahili. kwa hiyo kupitia jukumu hili Kiswahili kimekuwa
kinakua.
- Kutoa huduma za tafsiri na
ukalimani kwa serikali, mashirika ya serikali na yasiyo yaserikali na
asasi nyingine. Kupitia tafsiri zinazofanywa
na BAKITA Kiswahili kimekuwa kikikuwa na kuenea.
- Kuchapisha jarida au toleo
linalohusu lugha na fasihi ya Kiswahili.
Machapisho haya ya BAKITA yanaendelea kukifanya Kiswahili kukua kwa
kuongeza msamiati mpya na hivyo watu wanaposoma machapisho hayo
wanajifunza msamiati mpya na hivyo kufanya Kiswahili kukua.
- Kushirikiana na mashirika ya
kitaifa, asasi na watu binafsi, kufuatilia, kushauri na kusimamia shughuli
zinazolenga kukuza Kiswahili nchini Tanzania.
- Kutoa ushauri kwa waandishi na
wachapishaji ili watumie Kiswahili fasaha. Kwa kufanya hivi matumizi bora ya Kiswahili yanakuwa
yanaimarika.
- Kushirikiana na Wizara ya Elimu
na Mafunzo ya Ufundi kuthibitisha vitabu vya Kiswahili vitakavyotumika
shuleni na vyuoni kabla havijachapishwa.
Hili pia ni jamabo linaloimarisha matumizi ya Kiswahili sanifu.
TAKILUKI
Taasisi ya Kiswahili na Lugha za
Kigeni (TAKILUKI) ilianzishwa mwaka 1979 kwa lengo la kukuza na kueneza lugha
ya Kiswahili ndani na nje ya Zanzibar, ili kutimiza lengo hilo TAKILUKI
inajishughulisha na kazi zifuatazo:
- Kuratibu na kuendesha mafunzo
ya lugha ya Kiswahili visiwani Zanzibar, kuendesha mafunzo ya lugha ya
Kiswahili kwa wazawa na wageni, kuhariri miswada mbalimbali ili
kuthibitisha ufasaha wa Kiswahili na kufanya tafiti za Kiswahili katika
Nyanja zake zote, hususani katika uwanja wa sarufi na fasihi.
- Pia TAKILUKI wana kazi ya
kuandaa istilahi za taaluma mbalimbali, kutoa huduma za taaluma
mbalimbali, kutoa huduma za tafsiri na ukalimani kwa lugha mabalimbali kwa
mashirika, idara, wizara, taasisi, kampuni na watu binafsi, kufundisha
lugha za kigeni na kuandika vitabu mbalimbali vya Kiswahili.
- Pia hujishughulisha na utoaji
wa ushauri wa kitaaluma kwa watunzi wa vitabu ili waweze kuandika kazi
zenye ubora, na kushirikiana na wadau wengine wa Kiswahili kama vile,
mashirika, wizara, taasisi, vyuo na watu binafsi katika kuendesha shuguli
za ukuzaji wa Kiswahili, mathalani kuandaa na kuendesha semina, warsha na
kozi fupifupi za Kiswahili.
- Vilevile hujishugulisha na
usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili katika
vyombo vya habari na katika shughuli mbalimbali za serikali na za kawaida.
TUKI/TATAKI
Majukumu ya TUKI ni pamoja na kuunda
sera muafaka za kustawisha Kiswahili na pia kufanya utafiti katika lugha ya
Kiswahili.
Majukumu mengine ya TUKI ni
kuhariri, kuchapisha vitabu na kutawanya vitabu na majarida ya kitaaluma katika
Kiswahili.
Kwa sasa TATAKI inatoa shahada ya
awali na uzamili katika lugha ya Kiswahili, kwa njia hii inawaandaa wataalamu
wa lugha ya Kiswahili ambao watatumika sehemu mbalimbali za ulimwengu
kufundisha lugha ya Kiswahili.
CHAUKIDU
CHAUKIDU ni kifupi cha Chama cha
Ukuzaji wa Kiswahili Duniani, makao makuu ya chama hiki kwa sasa yapo chuo
kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani
Madhumuni makuu ya CHAUKIDU ni:
Kuwajumuisha pamoja wakuzaji wa Kiswahili duniani kote kwa lengo la kuchochea
kasi ya malengo mahususi yafuatayo:
- Kukuza Kiswahili katika nyanja zote ambamo lugha hii inatumika au
inaweza kutumika na kuongeza ufanisi wa mawasiliano katika ufundishaji na
utafiti wa maarifa ya aina zote, uandishi/utangazaji wa habari, uandishi
wa vitabu, uchapishaji vitabu na majarida, utayarishaji wa safari za
mafunzo katika Afrika ya Mashariki na Kati, n.k.
- Kusambaza habari na matokeo ya
utafiti kwa kutumia machapisho
mbalimbali na teknolojia ya mtandao wa kompyuta juu ya vipengele
mbalimbali vya Kiswahili na masuala yanayohusiana na Kiswahili.
- Kuwajumuisha wanachama kwa ajili ya kubadilishana mawazo na tajiriba zao
katika masuala mbalimbali yanayohusu Kiswahili (k.v. uboreshaji wa
ufundishaji, utangazaji, utafiti, uandishi, nk.) kwa njia ya mkutano wa
kila mwaka, warsha au semina au kongamano maalumu, na hata kwa njia ya
mtandao.
- Kuelimisha umma juu ya umuhimu wa kujivunia, kuendeleza, na kuheshimu
Kiswahili.
- Kushauri ama kushinikiza serikali za nchi ambamo Kiswahili kinazungumzwa
kutambua thamani iliyobebwa na maliasili hii ili kuunda sera muafaka za
kukiendeleza kadri ya uwezo wake kwa manufaa ya maendeleo ya serikali na
watu wake kijamii, kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, kielimu, n.k.
CHAWAKAMA
CHAWAKAMA husimama badala ya Chama
cha Wanafunzi wa Kiswahili vyuo vikuu Afrika Mashariki. Chama hiki kilianzishwa
mwaka 2004 kwa lengo la kukuza na kueneza Kiswahili katika eneo lote la Afrika
Mashariki kupitia wanafunzi wanaosoma Kiswahili vyuoni. Wanachama wa chama hiki
ni wale wanosoma Kiswahili na hata wale wenye mapenzi ya lugha ya Kiswahili pia
wanaweza kujiunga na chama hiki.
Chama hiki kina utaratibu wa kuandaa
makongamano ambapo wanachama wake kutoka nchi zote za Afrika Mashariki hupata
fursa ya kukutana mara moja kila mwaka. Pamoja na utaratibu wa chama kuandaa
makongamano pia uanzishwaji wake umeambatana na malengo kadhaa ambayo ndiyo
dira inayoiongoza chama kwa mujibu wa katiba, malengo hayo ni haya yafuatayo:
- Kuwapa wanachama nafasi ya
kujadili, kuimarisha, kuendeleza na kukuza vipawa vyao vya lugha na fasihi
ya Kiswahili.
- Kuamsha ari ya mapinduzi ya
utamaduni wa lugha ya kiswahili.
- Kueneza lugha ya kiswahili
ndani na nje ya nchi.
- Kushirikiana na vyama vingine
katika juhudi za kuendeleza na kuimarisha lugha ya kiswahili ndani na nje
ya nchi wanachama.
- Kuwaunganisha wanafunzi wa
kiswahili Afrika Mashariki na kati katika kukikuza kiswahili.
- Kushirikiana na asasi
mbalimbali zinazojihusisha na ukuzaji na uenezaji wa kiswahili ndani na
nje ya nchi kama vile BAKITA, TATAKI, TAKILUKI, UWAVITA, CHAKAMA, BAKIZA
n.k.
- Kuchapisha kijarida cha chama
na machapisho mengine ili kusaidia kueneza taaluma ya kiswahili.
- Kuweka kumbukumbu ya wataalamu
wa kiswahili kwa nia ya kuwatumia katika kufanikisha malengo ya chama na
wadau wa Kiswahili.
- Kuratibu makongamano na
mijadala mbalimbali inayohusiana na taaluma ya kiswahili.
Pamoja na malengo hayo, lengo kuu la
chama hiki ni kueneza Kiswahili lakini sasa wanakienezaje? Wanachama wa chama
hiki ambao ni nchi wanachama wa jumuia ya Afrika mashariki wanakawaida ya
kuandaa makongamano kwa ngazi ya kitaifa na ngazi ya kimataifa.
Kwa ngazi ya kitaifa kila nchi
huandaa kongamano kila mwaka ambalo linawakutanisha wanachama wote kutoka vyuo
mbalimbali katika nchi husika. Katika kongamano hilo mada mbalimbali zinazohusu
lugha ya Kiswahili na mustakabali wake hujadiliwa lakini pia maazimio
mbalimbali huchukuliwa juu ya maendeleo ya chama. Sasa katika mijadala kama hii
inatoa nafasi ya Kiswahili kukua kwani makala mbalimbali huandikwa ambazo pia
husomwa na watu mbalimbali. Makala hizi pia zimekuwa zikichapishwa katika
majarida ya chuo husika na pia zimekua zikichapishwa mtandaoni ambapo hutoa
fursa kubwa kwa watu wengi zaidi kuzifikia na kusoma, hivyo kwa njia hiyo
Kiswahili kinakua kimeenea.
Dhima ya kila Asasi inayokuza
Kiswahili
Mafanikio na Changamoto
Zinazovikabili Vyombo vya Ukuzaji wa Kiswahili
Mafanikio
- Vyombo vya ukuzaji wa Kiswahili
vimejitahidi sana kukuza lugha ya Kiswahili, kwa hali ya Kiswahili ilivyo
sasa ni matokeo ya juhudi za vyombo hivyo. Mafanikio ya vyombo hivyo ni
pamoja na haya yafuatayo:
- Machapisho ya lugha ya
Kiswahili ni mengi sana nchini na nje ya nchi, kufanya mafunzo ya
Kiswahili, kukua kwa matumizi ya Kiswahili na kuongezeka kwa idadi ya
watumiaji wa Kiswahili nchini.
- Matumizi ya lugha ya Kiswahili
katika sehemu rasmi hasa katika ofisi za serikali na ofisi za watu binafsi
inadhihirisha mafanikio ya jitihada za vyombo hivi kuhimiza matumizi ya
lugha ya Kiswahili.
- Kufundshwa kwa lugha ya
Kiswahili kama taaluma kwa ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu.
Hizi ni jitihada za TATAKI katika kuhakikisha kunapatikana wataalamu wa
lugha ya Kiswahili, hivi sasa TATAKI wanafundisha lugha ya Kiswahili kwa
ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu.
- Matumizi ya lugha ya Kiswahili
katika vyombo mabalimbali vya kimataifa, matumizi ya lugha ya Kiswahili
katika vikao vya Umoja wa Afrika na pia ufundishwaji wa lugha ya Kiswahili
katika vyo mabalimbali Duniani ni ishara tosha ya kuonesha mafanikio ya
jitihada za vyombo vya ukuzaji na uenezaji wa Kiswahili.
Changamoto
- Vyombo hivi vinakabiliwa na upungufu
wa wataalam. Wataalamu wengi waliobobea katika taaluma za Kiswahili
wanakimbilia nje ya nchi wakidhani huko ndiko kuna maslahi mazuri zaidi.
- Upungufu wa fedha za kuendeshea
shughuli za ukuzaji wa Kiswahili katika vyombo hivi pia limekuwa ni tatizo
sugu. Kwa hiyo shughuli za ukuzaji wa Kiswahili zinakuwa zinakwenda
taratibu.
- Taasisi hizi pia zinashindwa
kujitangaza vizuri kutokana na kwamba hazina vyombo vya habari binafsi
ambavyo vingeweza kutumika kutangaza shughuli zao. Jambo hili
limesababisha vyombo hivi kushindwa kutoa elimu ya Kiswahili kwa kutumia
vyombo vya habari kutokana na kwamba gharama za kufanya hivyo ni kubwa.
- Vyombo hivi baadhi havina ofisi
za kudumu, na hivyo kuhamahama jambo ambalo linaathiri utendaji kazi wa
vyombo hivyo.
MADA YA TATU: UHAKIKI WA
KAZI ZA FASIHI ANDISHI
Uhakiki wa Ushairi,
Tamthiliya na Riwaya
Dhana ya Uhakiki
Fafanua vipengele vya uhakiki
Uhakiki ni kitendo cha kutathmini,
kueleza, kuainisha na kutoa maoni juu ya kazi fulani ya fasihi kwa kuongozwa na
kaida maalum. Kwa kiwango cha elimu ya sekondari mhakiki anafanya kazi ya
uhakiki ili kuonesha mambo yanayojitokeza kama vile, dhamira, migogoro, ujumbe,
falsafa, mtazamo, msimamo n.k
Dhima ya Mhakiki na Nafasi ya Mhakiki
Uhakiki ni kazi ambayo ina mchango
mkubwa sana katika kazi za fasihi. Kwa msingi huo uhakiki una dhima zifuatazo:
- Husaidia wasomaji kuilewa kazi
ya fasihi kwa urahisi;Watunzi
wa kazi za fasihi hutofautiana katika matumizi ya lugha na taswira, hivyo
mhakiki anapofanya kazi ya uhakiki anamsaidia msomaji kuelewa vipengele
hivi kwa kuvifafanua kwa lugha rahisi.
- Husaidia ukuaji wa kazi za
fasihi;Mhakiki anapoonesha ubora na
udhaifu wa kazi ya mtunzi fulani, watunzi wengine pia watafunguka kifikra
na kutunga kazi iliyobora zaidi.
- Uhakiki hukuza uelewa wa
mhakiki; Kwa kuhakiki kazi mbalimbali
za fasihi, mhakiki hujiongezea maarifa ya lugha pamoja na mambo yanayotokea
katika jamii.
Nafasi ya Mhakiki
Mhahiki ana nafasi kubwa katika kazi
za fasihi, Mhakaki ndiye anafafanua kazi ya fasihi ili hadhira iweze kumwelewa
vizuri mtunzi wa kazi hiyo. Kwa hiyo hapa mhakiki anasaidia kurahisisha
mawasiliano kati ya hadhira na mtunzi.
Vilevile mtunzi huwaonyesha watunzi
ubora na udhaifu wa kazi zao. Kwa kufanya hivyo huwawezesha watunzi kufanya
kazi bora zaidi.
Hatua za Kufuata wakati wa Kufanya
Uhakiki
Vilevile mtunzi huwaonyesha watunzi
ubora na udhaifu wa kazi zao. Kwa kufanya hivyo huwawezesha watunzi kufanya
kazi bora zaidi.
Kwanza ni kuisoma kazi ya fasihi;
hapa mhakiki anatakiwa kuisoma kazi husika ya fasihi kwa kina na kuielewa
vizuri.
Pili ni kuainisha na kuchambua mambo
muhimu yanayojitokeza katika kazi hiyo katika vipengele vya fani na maudhui.
Tatu ni kutoa tathimini au kuelezea
ubora na udhaifu wa kazi inayohusika.
UHAKIKI WA MASHAIRI
Shairi ni utungo wa kisanaa wenye
mpangilio maalum wa lugha ya mkato unaowasilisha mawazo au ujumbe kuhusu
mwanadamu au mazingira yake na hufuata utaratibu fulani.
Mashairi yapo ya aina mbili:
- Mashairi huru
- Mashairi ya arudhi
Mashairi ya arudhi
Haya ni mashairi yanayofuata kanuni
za kimapokeo au arudhi za utunzi wa mashairi. Arudhi/kanuni hizi ni pamoja na:
- Kugawika kwa shairi katika beti
- Beti kuwa na idadi maalum ya
mishororo.
- Mishororo ya ubeti kugawika
katika vipande
- Mishororo kuwa na ulinganifu wa
mizani
- Shairi kuwa na urari wa vina
- Shairi kuweza kuimbika / kuwa
na mahadhi au mapigo.
- Kuwepo kwa kipokeo katika
shairi
- Kuwa na mtiririko wa mantiki na
mawazo au muwala
- hairi kuwa na utoshelezo wa
beti / kujisimamia kimaana.
Mashairi huru
Pia hujulikana kama mashairi ya
kimapinduzi. Haya ni mashairi yasiozingatia lazima ya arudhi na hivyo huwa na
muundo huru. Sifa zake kuu huweza kuwa:
- Lugha ya muhtasari
- Lugha yenye mahadhi
- Lugha ya kisanii iliyo na
mafumbo na taswira
- Mara nyingine hugawika katika
beti.
- Mishororo kamilifu
(inayojitosheleza) na ile isiyo kamilifu (mishata)
Sifa za Mashairi
Mashairi huwa na sifa maalum
zinazoyatambulisha kama kazi ya kishairi, yawe ya kimapokeo au kimapinduzi.
Sifa hizi ni kama vile:
- Mashairi hutumia lugha ya mkato
/ muhtasari
- Ni sanaa au kazi iliyobuniwa
kwa ufundi
- Huwa na mpangilio maalum
kuanzia mistari hadi beti.
- Hutumia lugha teule na msamiati
teule uliosheheni tamathali, taswira na jazanda.
- Mashairi huwa na sifa ya kuweza
kuimbika hivyo shairi ni wimbo na wimbo ni shairi.
Dhima ya mashairi
- Kupasha ujumbe kwa hadhira kwa
njia ya upole na mvuto
- Kuelimisha na kuzindua jamii.
- Kuendeleza na kukuza kipawa cha
utunzi.
- Kuhifadhi msamiati wa lugha ya
Kiswahili na Sanaa ya fasihi.
- Kuburudisha hadhira na
wasomaji.
- Kuwasilisha hisia za ndani za
mtu na mawazo
Hatua za uhakiki wa mashairi
- Soma shairi polepole na kwa
makini kupata maana ya jumla.
- Soma shairi tena kwa utaratibu
ukizingatia maneno na vipande mbalimbali na kuchunguza maana ya kila
mojawapo
- Pitia maswali yote kwa makini
ukitilia maanani aina ya majibu yanayotarajiwa.
- Soma shairi tena ukipigia
mstari kwa penseli sehemu zinazoelekea kujibu maswali.
- Toa majibu kamilifu kulingana
na swali kwa lugha ya mtiririko.
Vipengee vya Uchambuzi Wa Mashairi
- Anwani/kichwa cha shairi – Huwa ni muhtasari wa shairi katika neno au sentensi
moja. Anwani ni kidokezo muhimu cha kinachozungumziwa katika shairi. Anwani
huweza kuwa ya moja kwa moja, fumbo, kinaya, kibwagizo au sehemu ya
kibwagizo. Ikiwa shairi halina anwani, basi lipewe anwani inayoafikiana na
maudhui au dhamira kwasentensi isiyozidi maneno 6.
- Maudhui – Haya ni masuala makuu au mambo muhimu yanayohusu
mwanadamu au mazingira yake yanayozungumziwa katika shairi. Kwa mfano:
malezi, siasa, usalama, unyanyasaji, ufisadi n.k. Maudhui hung’amuliwa kwa
wepesi kutokana na kisa kilichomo katika shairi.
- Dhamira / shabaha - Ni lengo kuu la mshairi katika kusanifu utungo wake.
Dhamira ya mtunzi huwa ni ujumbe kwa kifupi anaoutambua msomaji kutokana
na mwelekeo wa usemaji wa mtunzi katika shairi. Mfano: Baada ya
kusoma shairi, unaweza kung’amua mtunzi alitaka kusisitiza kauli kuwa uongozi
mbaya haufai, misitu ni uhai n.k. Dhamira hutokana
na mwelekeo wa mawazo ya mshairi au falsafa yake.
- Mbinu na tamathali za lugha - Ni mbinu za uandishi na tamathali za usemi
zilizotumiwa na mshairi katika shairi. Mfano:Mazda / ziada / zidi -
kurefusha maneno;enda kuwa enenda. Inksari / muhtasari - Ni
kufupisha maneno;aliyefika kuwa alofika. Utohozi – Mbinu ya
kugeuza msamiati / maneno ya lugha geni ili yaandikike na kutamkika kana
kwamba ni ya Kiswahili. Mfano: Time - taimu; One – Wani. Mbinu hii
vilevile huitwa ukopaji au uswahilishaji.
Taarifa Muhimu za Mwandishi wa kila Kitabu
Mwandishi wa fasihi ni mtu anaeweza
kubuni kazi ya fasihi na kuiweka katika maandishi. Unaposoma kazi za fasihi ni
lazima ujue taarifa muhimu za mwandishi wa kazi hiyo, ambazo ni jina, kwa
sababu kila utakapokua unajibu swali ni lazima utaje jina la mwandishi wa
kitabu. Falsafa na utamaduni kujua msimamo wake, na muundo kujua mpangilio wa
matukio, mtindo kujua upekee wake na matumizi ya lugha.
MADA YA NNE: KUTUNGA KAZI ZA
FASIHI ANDISHI
Utungaji wa Mashairi
Mambo ya Kuzingatia katika Utungaji
wa Mashairi
Utungaji/uandishi wa kubuni ni ule
unatokana na hisia ambazo zinamsukuma mtunzi ili atunge kazi yake. Hisia
zinaungana na wazo ambapo vitu hivyo vinamsumbua akilini na kumkosesha raha.
Mwandishi wa kubuni anataka aliwasilishe wazo lake ili hadhira ifahamu
kilichopo moyoni mwake. Mwandishi hukosa usingizi na hivyo hulazimika kuamka na
kuandika kile kinachomsukuma akilini mwake.
Uandishi wa kubuni unamtaka mtunzi
atumie milango yake ya fahamu kinagaubaga. Kuna milango ya fahamu mitano ambayo
ni pamoja na: kuona, kunusa, kusikia, kuhisi, na kuonja.
- Kuona: je, mhusika unayemfikiria kichwani mwako unamwonaje?
Umbo lake ni la kuvutia au kuchusha? Je, macho yake yakoje – je ni ya
golori au la? Ni makubwa au madogo? Je, ni mlemavu wa macho?
- Kunusa: pua zako zinakufanya usikie harufu gani? Je, ni harufu
mbaya au nzuri? Je, ni uvundo au marashi? Je, mhusika wako ananuka kikwapa
au uturi? Je, ananuka mdomo?
- Kuhisi: je, unapokaa karibu naye unajihisi nini? Je, unapata
mhemko wowote au huhisi chochote? Je, akikupapasa mwilini mwako unajisikia
nini? Akikugusa bega unajisikia nini?
- Kuonja: je, ukiweka kitu hicho mdomoni unaonjaje – ni chungu
au tamu? Je, ina pilipili au masala? Je, kuna chumvi au sukari? Je, kitu
hicho kina ukakasi au uchachu?
- Kusikia: je, sauti unayoisikia ikoje? Inamtoa nyoka pangoni?
Inakufanya ukose usingizi? Je, ni sauti nzuri au mbaya? Ni nyororo au
nzito? Kama ni sauti ya muziki – je, iko chini au juu (kelele)?
Uzoefu wa Mwandishi
Uzoefu ni hali ya kukaa au
kujishughulisha na jambo au kitu kwa muda mrefu.
Mwandishi ana uzoefu (uzoevu) wa
kukabiliana na maisha kwa kiasi gani? Je, ni matatizo gani ambayo umekutana
nayo katika maisha yako? Je, ni mafanikio gani umekutana nayo katika maisha
yako? Kwa mfano, katika ajali ya MV Spice (2011) kuna baadhi ya watu
waliokolewa na magodoro ya Tanzania? Magodoro haya yana nailoni na je kama
yasingekuwa na nailoni? Uzoevu/uzoefu wako ukoje?
Uchunguzi/utafiti
Uchunguzi unapaswa ufanywe na
mwandishi ili aweze kuandika jambo au tukio bila kuongopa. Kwa kufanya
udanganyifu, mwandishi atapoteza imani yake kwa wasomaji wa kazi zake.
Uchunguzi ili ufahamu au ujue mtu,
mnyama, mdudu na kadhalika – anatembeaje, anakulaje, analalaje, anaishije,
anachekaje, analiaje, anazaaje, anahusianaje na wenzane na mazingira yake? Haya
ni maswali muhimu katika kumwezesha mtunzi kufanya utafiti wa kina ili ajue
kitu anachotaka kukiandika akiandikaje na akiwasilishaje ili aweze kuikamata
hadhira yake.
Mwandshi baada ya kuzingatia mambo
haya sasa anaweza kuanza kutunga kazi yake. Hapa sisi tutajikita zaidi katika
utunzi wa mashairi. Kabala hatujaenda katika hatua ya utunzi ni muhimu kujua
dhana ya shairi kwa ujumla wake, na baada ya hapo tutakuwa tumekwisha pata
maarifa yakutosha juu ya mashairi ambayo yatatuwezesha kutunga mashairi.
Dhana ya shairi
Shairi ni kipande cha maandishi
kilichopangwa kwa utaratibu katika mistari. Sauti za silabi
hufanana zikiwa kati au mwisho mwa mstari. Maandishi hayo
yakisomwa huleta ujumbe na hisia fulani ya kimaisha.
Mpango wa maneno ya shairi, ambao
huweza kuimbwa hutoa picha wazi, maana halisi na burudani ya kimuziki. Nyimbo
nyingi za makabila zimepangiliwa kishairi ijapokuwa hazikuandikwa
Mashairi yana umbo ambalo huonekana
kwa mpangilio wa sauti na idadi ya maneno katika mistari. Umbo hili
hutofautisha shairi na tenzi. Kuna mambo kadhaa yanayotakiwa kufahamika kuhusu
shairi, nayo ni:
- Beti – Kifungu kimoja cha shairi ambacho kina uzani
sawa.
- Vina – Ni mwisho wa mistari ambayo huwa na silabi zenye
sauti ileile mwishoni mwa sentensi.
- Mizani – Ni idadi zilizo sawa za silabi katika kila mstari,
ubeti hadi ubeti.
- Kituo – Huu ni mstari wa mwisho wa ubeti. Kuna vituo vya
aina tatu:Kituo cha bahari – ni mstari unaotoka mwanzo hadi mwisho
bila kubadilika katika kila ubeti;Kituo cha kimalizio – ni kituo
ambacho mstari wa mwisho maneno yake hubadilika ubeti hadi ubeti;Kituo
nusu bahari – ni mstari wa mwisho ambao maneno yake nusu hubadilika na
nusu hubaki kama ulivyo ubeti hadi ubeti.
Katika mashairi (ya kimapokeo), kila
mstari lazima uwe umekamilika na ubeti uwe na maana kamili.
Vipengele vya fani katika mashairi
Vipengele vya fani katika shairi ni
pamoja na:
- Jina / anwani
- Mandhari
- Wahusika
- Muundo –tathnia, tathlitha,
tarbia, tathamisa, sabilia n.k
- Mtindo – pindu, msisitizo, beti
kubadilishana vina, kurudiwa kipande kizima cha mstari wa mwisho kikiwa ni
chanzo cha ubeti unaofuatia.
Vipengele vya Maudhui kati mashairi
- Vipengele vya maudhui ni pamoja
na: migogoro, ujumbe, falsafa, msimamo, mtazamo, na dhamira za mwandishi.
- Matumizi ya ushairi ni pamoja
na: kuomboleza, kubembeleza, kuliwaza, kufundisha, kuburudisha, kukosoa,
na kadharika.
Baada ya hapa sasa unaweza kuanza
kutunga shairi lako la kwanza.
MADA YA
TANO: ANDISHI
Uandishi wa Insha za
Kiada
Insha ni kifungu cha maandishi
kilichoandikwa kutokana na mtazamo wa mwandishi katika kujadili juu ya mada
fulani. Mwandishi anaweza kuandika kuipinga mada hiyo au kuishadidia mada hiyo.
Kuna aina mbili za insha, insha za kaida (zisizo za kisanaa) na insha za kisanaa.
Insha za kaida ni insha zinazotumia lugha ya kawaida kuelezea mambo
mbalimbali katika jamii, mfano juu ya mazingira, uchumi, biashara, historia
n.k.
Muundo wa Insha za Kaida
Katika uandishi wa insha, muundo
wake unakuwa na vitu vifuatavyo:
- Kichwa cha insha; kichwa cha insha hudokeza kile ulichokijadili katika
insha yako. Kwa mfano: Madhara ya matumizi ya madawa ya kulevya n.k
- Utangulizi; Mambo yaliyopo katika utangulizi ni pamoja na kutoa
fasili ya maneno muhimu na kuelezea kwa muhtasari mambo ambayo utakwenda
kuyajadili katika insha yako.
- Kiini cha insha; katika kiini ndipo kuna maelezo ya kina juu ya kile
unachokijadili katika insha yako, maelezo haya yanakuwa katika aya kadhaa
kulingana na idadi ya hoja ulizonazo katika mjadala wako.
- Hitimisho; hapa ndipo kuna muhtasari wa kile kilichojadiliwa
katika kiini cha insha au inaweza kuwa ni msimamo juu ya kile
kilichohadiliwa katika insha.
Mambo ya kuzingatia katika uandishi
wa insha
Taratibu za uandishi zinapozingatiwa
insha pia itasomeka vizuri na pia itakuwa na mtiririko mzuri wa mawazo.
- Epuka kutumia vifupisho vya
maneno visivyo rasmi.Uandishi
wa insha ni suala rasmi, kwa hiyo katika uandishi wake inatakiwa
kuzingatia kuepuka kutumia vifupisho ambavyo sio majumui yaani
havijulikani. Kwa mfano maandishi kama, xamahani (samahani), ckatai
(sikatai) na mengine yafananayo kama hayo ni lazima yaepukwe katika
uandishi wa insha.
- Andika utangulizi unaovuta
umakini wa msomaji. Hiki
ni kipangele cha muhimu sana, msomaji anapoona kwamba kwenye utangulizi
hakuna kitu kinachomvutia hataendelea kuhangaika kusoma insha hiyo.
- Andika kiini cha insha kwa
mpangilio mzuri Unatakiwa kuandika insha yako
katika mpangilio mzuri huku kila wazo kuu likipewa aya yake na kuwepo na
mtiririko mzuri wa mawazo.
- Andika hitimisho la insha
likiwa linahitimisha mawazo yaliyokwishajadiliwa katika kiini.Hakikisha unapofanya hitimisho epuka kudokeza wazo
jipya ambalo linazua mjadala mpya, hakikisha hitimisho lako linabeba
mawazo uliyokwisha yajadili katika insha yako na wala yasiwe mawazo yanayotoka
nje ya kile ulichokijadili.
Uandishi wa Hotuba
Hotuba ni insha ambayo hutoa maneno
halisi ya mzungumzaji/kiongozi anapozungumzia hadhira, kuhusu jambo fulani.
Insha ya hotuba huandikwa katika hali ya usemi halisi na mwandishi hatakiwi
kuweka alama za kunukuu anapoanza insha yake.
Hotuba inaweza kutolewa na kiongozi
wa kisiasa, utawala, kidini, kikundi, shirika fulani, daktari, n.k. Hadhira
katika hotuba husheheni wageni waalikwa, wanachama, wafuasi, wananchi, n.k
ambao wanahusishwa katika mada inayorejelewa katika hotuba hiyo.
Muundo wa Hotuba
Hutuba inakuwa na muundo ufuatao:
Anwani
Anwani, mada au kichwa cha hotuba
hurejelea mada ya hotuba. Pia mada inaweza kutaja hadhira.
- Hotuba ya Waziri wa Afya kuhusu
madhara ya ukimwi kwa wananchi.
- Hotuba ya Mwalimu Mkuu kwa
Wazazi
Utangulizi
- Anza hotuba yako kwa kuwatambua
waliohudhuria mkutano (hadhira).
- Wataje kwa majina/vyeo vyao
kuanzia yule wa cheo cha juu hadi wa chini, mabibi na mabwana. Kumbuka
kwamba hauhitajiki kuwasalimia. Kuwatambua kwa majina pekee kunatosha.
- Jitambulishe kwa hadhira yako
hasa ikiwa unazungumzia hadhira isiyokujua au wageni.
- Tanguliza mada yako.
Kwa mfano:
Waziri wa Kilimo, Mkuu wa Wilaya,
Mhe. Mbunge, wanachama wa kikundi hiki cha Mazingira, mabibi na mabwana. Ni
matumaini yangu kwamba nyote mu buheri wa afya. Mimi ni mwakilishi wa Kikundi
cha Mazingira na jioni ya leo kuna jambo muhimu ambalo ningependa sote
tulifahamu ili kuboresha mazingira yetu kwa …
Kiini
- Hakikisha kuna mtiririko wa
hoja kuanzia mwanzo hadi mwisho
- Ujumbe wako wote unapaswa kuwa
katika usemi halisia wala si wa taarifa.
Tamati
- Hakikisha kwamba mwisho wa
hotuba yako unatambulika.
- Unaweza kumaliza kwa shukurani
Uandishi wa Risala
Risala ni hotuba fupi inayosomwa
mbele ya kiongozi kwa niaba ya kundi fulani la watu hasa hasa wanafunzi,
wafanyakazi, washiriki, wanachama, mafundi n.k ili kutoa maelezo ya haja zao
mbalimbali na mahitaji yao au kuonyesha msimamo wa kundi hilo kwa kiongozi.
Muundo wa Risala
Utanguizi
- Cheo cha kiongozi anayehusika
- Kundi linalowakilishwa
Kiini
- Maelezo ya hali halisi ya
maswala na msimamo wa kundi linalowakilishwa.
- Mapendekezso na hatua
zinazotakiwa kuchukuliwa.
Hitimisho
- Shukrani
Tanbihi: Kama vilivyosemwa awali risala ni hotuba fupi lakini
inachukua mambo muhimu tu na kuyaeleza. Hivyo risala yenyewe huwa ni maelezo ya
muhtasari kwa jambo linalohitaji maelezo marefu Katika hotuba. Utungaji wa
risala unahitaji uangalifu sana na lugha ya heshima iliyo wazi kueleweka kwa
kiongozi.
Mfano wa risala:
Ndugu Mgeni rasmi, Walimu, Wanafunzi
wenzetu, Wazazi, Wageni waalikwa, Mabibi na Mabwana.
Kwa niaba ya wanafunzi wa kidato cha
nne, tunayo heshima na furaha kubwa , kukukaribisha ili ushiriki nasi katika
siku hii muhimu na kusikia mafanikio mbalimbali kwa kipindi chote cha masomo
yetu hapa shuleni.
Shukrani zetu za pekee na za dhati
ziende kwa uongozi mzima wa Shule na walimu wetu wote kwa jinsi walivyojitoa
kwa moyo wa kutufundisha, hivyo tumefundishika vyema; kwasababu tupo tofauti
sana na tulivyokuja hapa mwezi januari 2009.
Ndugu mgeni rasmi, tulianza kidato
cha kwanza tukiwa wanafunzi 120; wasichana 60 na wavulana 60. Mpaka leo
tunapohitimu tupo wanafunzi 90; kati yao wavulana ni 43, na wasichana 47.
Wengine wameshindwa kuhitimu nasi siku ya leo kutokana na sababu mbalimbali
zikiwemo utoro, ujauzito na kuhama shule. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa
Rehema wa Baraka kwa ulinzi wake kwetu hadi leo hii tunahitimu kidato cha nne.
Ndugu mgeni rasmi, elimu hii ya
kidato cha nne imetupatia msingi mzuri wa kujiunga na Elimu ya juu, pia
imetujengea uwezo mzuri wa kujitambua na kufikiri, kufanya kazi vizuri na
kufanya maamuzi sahihi; pia imetuwezesha sisi wanafunzi kupata elimu ya mambo mbalimbali
kupitia masomo tunayo fundishwa hapa shuleni, mfano; tumepata elimu ya uraia,
historia ya mambo mbalimbali katika nchi yetu na dunia kwa ujumla, pia tumeweza
kupata uelewa kuhusu afya na magonjwa, usalama katika mazingira yetu, Kilimo,
Maumbile ya nchi, hali ya hewa, misitu, na viwanda. Vilevile tumeelewa umuhimu
wa kusoma vitabu mbalimbali kwa lengo la kupata ujuzi wa kuinua uchumi wetu wa
taifa.
Ndugu mgeni rasmi, mafanikio hayo
yamepatikana kwasababu ya ushirikiano mzuri kati yetu na walimu wetu. Tangu
tujiunge na shule hii tukiwa kidato cha kwanza tumefanya majaribio na mitihani
ya mara kwa mara jambo lililo tusaidia kuinua taaluma yetu.Tunawashukuru sana
walimu wetu, tuna waahidi kufanya vizuri katika mitihani yetu ya Taifa ya
kidato cha nne mwaka huu, na Mungu awabariki sana.
Ndugu mgeni rasmi, tumepata
changamoto mbalimbali wakati wa maisha yetu ya kielimu hapa shuleni, kama
ifuatavyo;
Ndugu mgeni rasmi, tuna changamoto
ya upungufu wa vitabu vya kiada na ziada; hii imepelekea kushindwa kujisomea
vizuri, kwani kitabu kimoja kinatumiwa na wanafunzi zaidi ya ishirini (20).
Ndugu mgeni rasmi, changamoto
nyingine ni upungufu wa vifaa vya maabara, hii inapelekea kuchangia kifaa
kimoja, hivyo tuna tumia muda mwingi sana kujifunza na kumuelewa mwalimu.
Ndugu mgeni rasmi, pia kuna
changamoto ya upungufu wa walimu, hasa wa masomo ya sayansi; hii imepelekea
kutomaliza ‘syllabus’ kwa wakati.
Ndugu mgeni rasmi, pia kuna
changamoto ya upungufu wa samani za shule, kama vile; madawati kwa ajili ya
wanafunzi, viti na meza kwa ajili ya walimu; hii imepelekea baadhi ya wanafunzi
wenzetu kukaa wawili kwenye dawati moja.
Ndugu mgeni rasmi, maji ni
changamoto hapa shuleni, kwani shule haina kisima cha maji, hii imepelekea
shule kununua maji kwa gharama kubwa, ambayo hayatoshelezi mahitaji ya shule,
kama vile usafi; hususani kwa upande wa vyoo, bila kuwa na maji ya kutosha
tutapata magonjwa ya mlipuko, kama vile kipindupindu.
Ndugu mgeni rasmi, changamoto ya
vifaa vya michezo; kama unavyojua kuwa michezo ni afya, shule yetu ina upungufu
mkubwa wa vifaa vya michezo kama vile; mipira ya miguu, pete na mikono, pia
hatuna milingoti ya chuma kwaajili ya magoli ya viwanja vya michezo yote
tunayocheza hapa shuleni.
Ndugu mgeni rasmi, tunashukuru
uongozi wa shule hii, walimu na wazazi ambao wamekuwa mstari wa mbele katika
kuchangia maendeleo ya shule yetu; kwa upande wa masomo ya sayansi; shule
imeweza kutenga chumba kimoja cha darasa kitumike kama maabara japo kuwa kuna
upungufu mkubwa wa vifaa.
Ndugu mgeni rasmi, tunayo matumaini
kwamba maombi yetu umeyasikiliza na utayaatekeleza, maana tunajua kwamba wewe
unaweza kupitia Hlimashauri unayo isimamia, asante sana.
Mwisho tunaomba msamaha wa dhati
toka moyoni mwetu kwa Walimu, Wanafunzi wenzetu na Wazazi pale tulipoenda
kinyume na matazamio yenu, kwani watu wakiishi pamoja tofauti lazima ziwepo,
tunatumaini mtapokea msamaha wetu, nasi hatuna jambo lolote baya kwenu.
Ndugu mgeni rasmi, tuna kushukuru
sana kwa kufika katika Mahafali yetu, kwani tunatambua kuwa unamajukumu mengi
ambayo umeyaacha na kuwepo hapa kwaajili yetu.
Uandishi wa kumbukumbu
za Mikutano
Kumbukumbu za mikutano ni rekodi
zinazowekwa na katibu wa mkutano wakati mkutano unapoendelea ili kuhifadhi
yanayojadiliwa na kukubaliana katika mkutano huo. Katibu anapaswa kufuatilia
mtindo maalum wa kuandika kumbukumbu hizo kulingana na mpangilio katika
mkutano.
Mambo ya Kuzingatia katika Uchukuaji wa Kumbukumbu za
Mikutano
Mambo ya kuzingatia katika uandishi
wa kumbukumbu ni kama yafuatayo:
- Kichwa cha kumbukumbu – Kichwa cha kumbukumbu kinapaswa kutaja mambo
yafuatayo: Ni mkutano wa akina nani? Unaandaliwa wapi? Unaandaliwa lini?
Unaanza saa ngapi? Mfano wa Kichwa cha Kumbukumbu: Kumbukumbu za Mkutano
wa Shirika la Msalaba Mwekundu Shuleni ulioandaliwa tarehe saba Agosti 2001
katika Ukumbi wa Mikutano kuanzia saa Tisa alasiri.
- Waliohudhuria – Andika orodha ya wote waliofika kwenye mkutano huku
kuanzia na yule mwenye cheo cha juu zaidi hadi kwa wanachama. Pia onyesha
vyeo vyao.
- Waliotoa Udhuru -Hawa ni wale walioomba ruhusa kutohudhuria mkutano
- Waliokosa kuhudhuria - Hawa ni waliokosa kuhudhuria mkutano, bila kutoa
udhuru)
- Waalikwa - Hawa ni wageni walioalikwa katika mkutano, k.v mlezi
wa chama, afisa wa kiutawala, n.k)
- Ajenda -orodhesha hoja zitakazorejelewa katika mkutano huo
Kuandika kumbukumbu
KUMB 1
|
Kumbukumbu ya kwanza huwa ni
kufunguliwa kwa mkutano na ujumbe kutoka kwa mwenyekiti.
|
KUMB 2
|
Kusomwa kwa kumbukumbu za mkutano
uliotangulia na kuthibitishwa kwa kumbu kumbu hizo kwa kutiwa saini.
|
KUMB 3
|
Maswala yanayoibuka kutokana na
kumbu kumbu zilizosomwa. (Kumbuka kutaja nambari ya kumbu kumbu hizo)
|
KUMB kuendelea
|
Maswala katika ajenda
|
KUMB ya Mwisho
|
Maswala mengineyo yasiyokuwa
kwenye orodha ya ajenda.
|
Tamati
|
Kufungwa kwa mkutano. Taja mkutano
ulifungwa saa ngapi; mkutano ujao utakuwa tarehe ngapi; kisha acha nafasi ya
kuthibitishwa kwa kumbu kumbu hizo katika mkutano utakaofuatia.
|
Mfano
KUMBUKUMBU ZA MKUTANO WA CHAMA CHA
KISWAHILI ULIOANDALIWA KATIKA CHUMBA CHA MIJADALA TAREHE 24 JUNE 2013 KUANZIA
SAA TATU ASUBUHI
Waliohudhuria
- Teddy Mbogela – Mwenyekiti
- Vaileth Matiko – Mweka hazina
- Iliashibu Masatu – Mkuu wa
utafiti
- Funk Kiduku – mwanachama
- Meta Mkorofi – katibu
Waliotuma Udhuru
- Bahatika Mashauri – Naibu
Mwenyekiti
- Ponea Kamgazi – Msimamizi wa
Mijadala
Waliokosa Kuhudhuria
- Zebedayo Chisege – Spika
- John Kumbikumbi – mwanachama
Waalikwa
- Mnoko Nokwe – Mwanahabari
- Dkt. Fikirini– Mlezi wa Chama.
Ajenda
- Uchapishaji wa jarida la
Kiswahili
- Shindano la kuandika insha.
- Kusajili wanachama wapya
KUMBUKUMBU 3/04/14 – KUFUNGULIWA KWA
MKUTANO
Mwenyekiti aliwakaribisha wanachama
wote na baada ya kuwatambulisha wageni, akawaomba washiriki wawe huru kuchangia
katika ajenda mkutano huu ili kuboresha chama.
KUMBUKUMBU 7/04/14 – KUREJELEA
KUMBUKUMBU ZA MKUTANO ULIOPITA
Katibu alisoma kumbukumbu za mkutano
wa mwezi Machi. Kumbukumbu zilikubaliwa na wanachama wote na kuthibitishwa na
mwenyekiti pamoja na katibu kwa kutia saini.
KUMBUKUMBU 10/04/14 – MASWALA IBUKA
KUTOKANA NA KUMBUKUMBU ZILIZOSOMWA
Mweka hazina alifahamisha mkutano
kwamba aliongea na mkuu wa idara ya Kiswahili kuhusu ufadhili kama tulivyokuwa
tumekubaliana katika KUMB 9/03/10 ya mkutano uliopita.
KUMBUKUMBU 12/04/14 – HAFLA YA
KISWAHILI
Iliripotiwa kwamba hafla ya
Kiswahili ambayo wanachama walikuwa wamealikwa kuhudhuria katika Shule ya
Sakata Academy haingeweza kufanyika kutokana na tamasha la muziki lilizokuwa
linaendelea katika shule hiyo. Wanachama waliokuwa wamejitayarisha kwa mashairi
waliombwa kuendelea kujifunza ili wayawasilishe muhula wa pili.
KUMBUKUMBU 15/04/14 – UCHAPISHAJI WA
JARIDA LA KISWAHILI
Wanachama walikubaliana:
- Kwamba chama kitaanza
kuchapisha jarida la Kiswahili
- Kwamba jarida litakuwa
likichapishwa mara moja kila muhula na kuuzwa shuleni
- Kwamba kila mwanachama
atachangia katika kuandika makala na kuuza nakala za jarida hilo.
- Kwamba paneli ya wahariri
lingeundwa ili kuongoza idara ya uchapishaji
- Kwamba hazina ya chama ina
fedha za kutosha kuzindua uchapishaji huo.
KUMBUKUMBU 17/04/14 – SHINDANO LA
KUANDIKA INSHA
Kila muhula wa pili, chama huandaa
shindano la kuandika insha ambalo wanafunzi wote hushiriki. Insha
zilizopendekezwa mwaka huu ni:
- “Jadili chanzo cha migomo
shuleni na namna ya kusuluhisha.”
- … … … … … … … … …
- … … … … … … … … …
- … … … … … … … … …
KUFUNGWA KWA MKUTANO
Mkutano ulifungwa saa kumi na nusu,
baada ya maswala yote kujadiliwa. Mkutano unaofuatia ulipoangwa kuwa tarehe
ishirini mwezi Mei, katika Ukumbi wa Muziki.
KUTHIBITISHWA KWA KUMBU KUMBU
______________
|
_____________
|
Mwenyekiti
|
Katibu
|
Tarehe:________
|
Tarehe:________
|
MADA
YA SITA: UFAHAMU
Ufahamu wa Kusikiliza
Ufahamu wa kusikiliza ni zaidi ya
kusikiliza tu kile kilichosemwa; badala yake ni uwezo wa mtu kuelewa maana ya
maneno anayoyasikia na kuweza kuhusiana nayo kwa namna fulani. Kwa mfano
mwanafunzi anaposikiliza hadithi, ufahamu mzuri wa kusikiliza humsaidia kuielewa
hadithi hiyo, kuikumbuka, kuijadili, na hata kuisimulia tena kwa maneno yake
mwenyewe.
Kujibu Maswali ya Habari
Uliyosikiliza
Ufahamu wa kusikiliza unahusisha
michakato kadhaa katika kuelewa na kupata maana ya kile kinachozungumzwa.
Michakato hii inahusisha:
- Kuelewa vizuri sarufi ya lugha
ile inayozungumzwa
- Kuelewa vyema maana ya maneno
ya mhusiaka anayezungumza
- Kuelewa sintaksia (muundo wa
maneno) ya sentensi kwa namna zinavyowasilishwa.
Katika ufahamu wa kusikiliza,
msikilizaji hana budi kuzingatia mambo yafutayo:
- Kuwa makini na kuelekeza akili
yote kwa mzungumzaji ili kuweza kusikia kila anachokisema.
- Kutilia maanani vidokezo vya
maana ili kubaini iwapo msemaji anaongeza jambo jipya, anatofautisha,
anafafanua au anahitimisha hoja.
- Msomaji anatakiwa kuandika
baadhi ya mambo anayoona kuwa ni ya muhimu ili kumasidia kukumbuka hapo
baadae.
- Kuwa makini na ishara mbambali
za mwili kama vile kurusha mikono, kutingisha kichwa, kutingisha mabega au
hata kupepesa macho. Ishara hizi huwa zinachangia kwa kiasi kikubwa kupata
maana katika mazungumzo.
Kufupisha Habari
Ili kuandika ufupisho mzuri wa
habari uliyoisikiliza yafuatayo hayana budi kuzingatiwa; kusikiliza habari kwa
makini ili kuielewa vizuri, kuandika mawazo makuu yanayojitokeza katika kila
aya, kuyaunganisha mawazo makuu na kuiandika habari kwa maneno yako, kuhesabu
idadi ya maneno kama inazidi na kuandika idadi hiyo mwisho wa ufupisho upande
wa kulia chini kidogo.
Zoezi
Soma habari kisha toa ufupisho wake
Ufahamu wa Kusoma
Ufahamu
wa kusoma ni ule mtu anaoupata kwa njia ya kusoma makala, kifungu cha habari,
kitabu au gazeti.
Kujibu Maswali kutokana na Habari
ndefu uliyosoma
Kuna vipengele viwili vinavyounda
mchakato wa ufahamu wa kusoma:
- Uelewa wa msamiati na
- Uelewa wa matini
Ili kuilelewa habari/matini ni
lazima msomaji awe na uwezo wa kuelewa msamiati uliotumika katika matini hiyo.
Endapo maneno yaliyotumika hayataeleweka vilevile matini yote hataeleweka.
Katika ufahamu wa kusoma, msomaji
anatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo:
- Kubaini mawazo makuu; msomaji anaposoma habari fulani au kitabu inatakiwa
ajiulize, Je, kinachoongelewa hapa ni nini? Ni jambo gani hasa
analolizungumzia mwandishi? Msomaji akiwa na maswali haya akilini mwake
basi itakuwa rahisi kwake kuielewa habari hiyo.
- Kuzingatia alama za uakifishi; msomaji ni lazima azingatie alama za uakifishi, kwa
kufanya hivyo itamsaidia kuelewa ujumbe wa habari hiyo na endapo
hatazingatia alama za uakifishaji anaweza kupotosha maana ya mwandishi.
- Kubaini maana ya maneno na
misemo mbalimbali;
habari nyingine huwa zina maneno ya kisanaa hivyo ni muhimu msomaji
kubaini maana ya maneno hayo katika muktadha wa habari hiyo, hii
itamsaidia kuelewa vyema maana ya mwandishi.
- Vilevile msomaji anatakiwa
kumakinikia kile anachokisoma, kila kipengele anachokisoma inampasa
akielewe vizuri.
Kwa kuzingatia haya yote msomaji
atakuwa na uelewa mzuri juu ya habari aliyoisoma na pia anaweza kufupisha
habari hiyo aliyoisoma.
Kufupisha habari
Kufupisha habari ni kuandika upya
habari uliyoisoma kwa maneno machache lakini bila kupotosha ujumbe wa habari ya
kwanza.
Ufupisho wa habari huwa na sifa
hizi:
- Huwa ni mfupi kuliko habari ya
mwanzo
- Huwa na ujumbe uleule uliokuwa
katika habari ya mwanzo
- Hujumuisha mawazo makuu
yaliyodondolewa kutoka kwenye habari ya mwanzo
- Mawazo haya sharti yapangwe
katika mtririko wenye mantiki
Hatua za kufuata katika kuandika
ufupisho
Ili kuweza kufanikiwa kufupisha
habari kwa ufanisi hatua zifuatzo sharti zifuatwe:
- Kuisoma au kuisilikiza habari
kwa makini ili kuielewa vizuri
- Kutambua na kubaini mawazo
makuu yanayojitokeza katika kila aya
- Kuyaunganisha mawazo makuu na
kuandika au kuelezea ufupisho wa habari hiyo kwa maneno yako mwenyewe bila
kupostosha maana ya habari ya kwanza.
- Kuhesabu idadi ya maneno ya
ufupisho ili kuyapunguza ikiwa yanazidi idadi iliyotakiwa.
- Kama muda unaruhusu pitia tena
habari ya mwanzo na pitia tena ufupisho ili kujiridhisha kuwa hujaacha
taarifa yoyote ya muhimu.
Kufupisha Habari ndefu uliyosoma
Ili kuweza kuandika ufupisho wa
habari ndefu uliyoisoma hatua zifuatazo sharti zifuatwe, kusoma habari kwa
makini na kuielewa vizuri, kubaini mawazo makuu, kuandika ufupisho wa habari
kwa maneno yako, kuhesabu idadi ya maneno na kupunguza yaliyozidi na kupitia
tena habari ya mwanzo na ya mwisho kama muda unaruhusu. Aidha ufupisho wa
habari huwa ni mfupi na una ujumbe uleule wa habari ya mwanzo.
5 Comments
good work. much respect........
ReplyDeleteGreat work.
ReplyDeleteAll the best mpella
ReplyDeleteUko vizuri asee
ReplyDeleteNice
ReplyDelete