KIDATO
CHA: TATU
MADA YA KWANZA: NGELI
ZA MANENO
Kuzielewa Ngeli
Upatanishi
wa Kisarufi katika Sentensi
Ngeli ni vikundi vya majina ya
Kiswahili. Ngeli za nomino ni utaratibu unaotumika kuweka nomino katika
matabaka au makundi yanayofanana.
Mfano:
- Maji yakimwagika hayazoleki
- Mayai yaliyooza yananuka sana
- Yai lililooza linanuka sana
- Maji liliomwagika halizoleki
Katika mifano hii tunaona kwamba
sentensi a, b na c ziko sahihi wakati sentensi d sio sahihi, hii ni kwa sababu
imekiuka upatanisho wa kisarufi. Kwa maana hiyo sentensi ‘a’ ipo katika ngeli
ya YA-YA na senthensi b na c zipo katika ngeli ya LI-YA. Sentesi d sio sahihi
kwa sababu nomino maji haina wingi, kwa hiyo haiwezi kuingia katika ngeli ya
LI-YA. Kwa msingi huu ngeli za nomino huzingatia sana upatanisho wa kisarufi.
Jedwali
lifuatalo huonesha ngeli za nomino kwa misingi ya upatanisho wa kisarufi.
NGELI
|
UFAFANUZI
|
MIFANO
|
A-WA
|
Ngeli hii inahusisha majina ya
viumbe hai kama vile wanyama, watu, wadudu, ndege n.k
|
Sungura mjanja ameumia
Sungura wajanja wameumia Mkuu anawasili
|
LI-YA
|
Majina yenye kiambaisha awali li-
katika umoja na ya- katika wingi huingia katika ngeli hii
|
Jambia la babu limepotea
Majambia ya babu yamepatikana
|
KI-VI
|
Ni ngeli ya majina ya vitu visivyo
hai, yanayoanza kwa KI- au CH- (umoja); na VI- au VY- (wingi). Pia ngeli hii
hujumuisha majina ya vitu vingine katika hali ya udogo k.v, kijito, kilima
|
Chakula kimekwisha
Vyakula vimekwisha Kijito kimekauka Vijito vimekauka
|
U-I
|
Huwakilisha majina ya vitu visivyo
hai, yaanzayo kwa sauti M- (umoja) na MI (wingi). Pia majina ya baadhi ya
viungo vya mwili huingia humu, kewa mfano mkono, mguu, mkia n.k
|
Mlima umeporomoka
Milima imeporomoka Mkono umevunjika Mikono imevunjika
Mto huu una mamba wengi Mito hii ina mamba wengi
|
U-ZI
|
Hurejelea majina ambayo huanza kwa
U- (umoja) na huchukua ZI- kama kiambishi kiwakilishi cha ngeli katika wingi.
Majina yenye silabi tatu au zaidi hubadilishwa kwa wingi kwa kutoa sauti /u/'
k.v ukuta-kuta. Majina ya silabi mbili huongezewa /ny/ katika wingi. k.v ufa
- nyufa
|
Ukuta umebomoka Kuta
zimebomoka Wimbo huu unavutia Nyimbo hizi zinavutia
Ufa umeonekana Nyufa zimeonekana
|
I-ZI
|
Hutumiwa kwa majina yasiyobadilika
kwa umoja wala kwa wingi lakini huchukua viambishi viwakilishi tofauti: I-
(umoja) na ZI- (Wingi).
|
Nyumba imejengwa
Nyumba zimejengwa Salam imefika Salam zimefika
|
U-YA
|
Ngeli hii inajumuisha nomino
ambazo zina kiambishi awali u- katika umoja na ma- katika wingi.
|
Ukuu umekuponza
Makuu yamekuponza Unyoya unapepea Manyoya yanapepea
|
KU
|
Majina yanayotokana na vitenzi
yanayoanza na ku- (vitenzi-jina)
|
Kusoma kwako kumekusaidia
Kuchelewa kumemponza
|
PA/MU/KU-
|
Huonesha mahali
|
Amekaa pale palipo
na wadudu wengi Amelala mule mulimojaa siafu.
Amepita kule mbali
|
Baadhi ya matumizi ya ngeli ni
pamoja na haya yafuatayo:
- Hutumika kupanga majina ya lugha katika makundi
yaliyoshikamana na kutofungamana kutokana na kigezo muhimu.
- Hutumika kutambulisha maumbo ya umoja na wingi katika
majina na vivumishi.
- Hutumika katika upatanishi wa kisarufi katika sentensi.
- Hutumika katika kuonyesha uhusiano uliopo baina ya
lugha za Kiswahili na lugha zingine.
Habari
zenye Upatanishi wa Kisarufi
Baadhi ya matumizi ya ngeli ni
pamoja na haya yafuatayo:
- Hutumika kupanga majina ya lugha katika makundi
yaliyoshikamana na kutofungamana kutokana na kigezo muhimu.
- Hutumika kutambulisha maumbo ya umoja na wingi katika
majina na vivumishi.
- Hutumika katika upatanishi wa kisarufi katika sentensi.
- Hutumika katika kuonyesha uhusiano uliopo baina ya lugha
za Kiswahili na lugha zingine.
MADA YA PILI:
MJENGO WA TUNGO
Tungo
Tungo ni kipashio cha kisarufi kilichoundwa kwa kuunganisha
pamoja vipashio vidogovidogo vilivyo chini yake. Au tungo ni neno au kikundi
cha maneno ambacho hudokeza taarifa fulani ambayo huweza kuwa kamili au isiyo
kamili.
Kwa maana hii, tungo hujengwa na
vipashio vidogovidogo kama vile mofimu kuunda neno, neno kuunda kirai, kirai
kunda kishazi na kishazi kuunda sentensi. Kama tulivyokwisha kuona hapo juu
tungo huanzia neno; rejea aina za tungo.
Aina
za tungo
Tungo neno: Tungo neno ni tungo ambayo huundwa na vipashio vidogo zaidi
ya neno ambayo ni mofimu au fonimu. Mfano; anacheza, kakimbia.
Tungo Kirai: ni kipashio cha kimuundo chenye neno moja au zaidi lakini
ambacho hakina muundo wa kiima kiarifu. Mfano; mtoto mzuri, kiyama chake,
bondeni
Tungo kishazi:Kishazi ni tungo yenye kitenzi ambacho chaweza kujitosheleza
na kukamilisha ujumbe uliokusudiwa na mzungumzaji au kuwa na kitenzi
kisichoweza kujitegemea chenyewe.
Kirai
na Uainishaji wake
Dhana ya kirai itaeleweka vizuri kwa
kuzingatia sifa zake zifuatazo:
- Kirai huwa ni kipashio cha kimuundo kisichokamilika;
yaani ni kipashio kisichokuwa na muundo wa kiima – kiarifu kama zilivyo
sentensi ambazo zinahusisha mtendaji wa tendo na tendo linalotendwa.
- Kirai huainishwa kimuundo kulingana na neno kuu la
kirai husika.
- Kirai ni tungo, yaani ni aina moja wapo ya tungo, aina
nyingine za tungo ni neno, kishazi na sentensi.
- Kirai hudokeza maana, lakini maana hiyo si kamili.
- Maneno katika kirai lazima yapangwe kimantiki kwa
mpangilio unaokubalika katika sarufi ya lugha husika. Japo virai
huainishwa kimuundo, huweza kutumika kutekeleza majukumu mbalimbali ya
kisarufi. Kirai huweza kutokea upande wowote, wa kiima au kiarifu katika
sentensi. Kirai ni kikubwa kuliko neno
Kama tulivyobainisha hapo juu aina
ya virai hukitwa katika aina za maneno ambazo ndizo chimbuko la mahusiano
maalumu ndani ya vipashio hivyo.
- Kirai nomino (KN); Ni
kirai ambapo neno lake kuu ni nomino. Ni kirai ambacho muundo wake
umekitwa kwenye nomino au mahusiano ya nomino na neno au mafungu ya
maneno.
- Kirai kitenzi (KT);
Kirai-kitenzi ni kirai ambacho kimekitwa katika kitenzi au katika
mahusiano ya Kitenzi na neno au mafungu mengine ya maneno. Hii ina maana
kuwa neno kuu katika aina hii ya virai huwa ni kitenzi.
- Kirai kivumishi (KV);
Kirai-kivumishi ni kirai ambacho muundo wake umekitwa katika kivumishi.
Kwa kawaida muundo huu huwa ni wa kivumishi na neno au fungu la maneno
linaloandamana nacho.
- Kirai Kielezi (KE);
Tofauti na aina nyingine ya virai miundo ya virai vielezi haielekei
kukitwa kwenye mahusiano ya lazima baina ya neno kuu (yaani kielezi) na
neno au fungu la maneno linaloandamana nalo. Badala yake miuundo
inayohusika hapa ni ya maneno ambayo hufanya kazi pamoja katika Lugha kama
misemo, neno au maneno yanayofuata neno lililotangulia yakifafanua zaidi
neno hilo.
- Virai viunganishi (KV); Ni kirai ambacho muundo wake umekitwa katika mahusiano
baina ya kwa na katika, au kwenye na fungu la maneno linaloandamana nacho.
Kwa maneno mengine kirai hicho ni kile ambacho neno kuu ni kiunganishi.
Tungo
kishazi
Kishazi ni tungo yenye kitenzi
ambacho chaweza kujitosheleza na kukamilisha ujumbe uliokusudiwa na mzungumzaji
au kuwa na kitenzi kisichoweza kujitegemea chenyewe.
Sifa za kishazi
- Kishazi hupatikana katika/ ndani ya sentensi.
- Lazima kishazi kiwe na kitenzi, sehemu yoyote ya
sentensi isiyo na kitenzi, haiwezi kuwa kishazi. Kishazi huru hutawaliwa
na kishazi kikuu na kishazi tegemezi hutawaliwa na kishazi tegemezi.
- Baadhi ya vishazi huweza kujitegemea kama sentensi hata
vikiondoshwa katika muktadha wa sentensi kuu. Kishazi kinachoweza
kujisimamia kama sentensi huitwa kishazi huru kikiwa ndani ya sentensi kuu
na huitwa “sentensi sahili” kikiwa sentensi inayojitegemea.
- Baadhi ya vishazi haviwezi kujitegemea kama sentensi
ikiwa vitaondoshwa katika muktadha wa sentensi kuu.
- Vishazi vingi, hata vishazi huru huwa na kiima dhahiri.
- Kishazi kwa kawaida, hasa kishazi huru huwa na kitenzi
kimoja kikuu.
- Kitenzi hicho huweza kuandamana na kitenzi kisaidizi.
Pia, kitenzi katika kishazi huweza kuwa kitenzi kishirikishi.
- Kishazi hutekeleza majukumu mbalimbali ya kisarufi.
- Tofauti ya kishazi na sentensi ni kwamba kishazi
hupatikana ndani ya sentensi lakini sentensi hujisimamia kimuundo na
kimaana.Kishazi huwa na kiarifu kimoja na kiima kimoja, Lakini sentensi
huweza kuwa na kiima kimoja.
Aina za vishazi
- Vishazi huru:
Kishazi huru ni kishazi kinachotaewaliwa ka kitenzi kikuu, ambacho kwa
kawaida hutoa ujumbe kamili usiohitaji maelezo zaidi ya kukamilisha maana.
Ni kishazi ambacho hata kikiondolewa katika muktadha wa sentensi ambamo
vimejikita huweza kujitegemea kama sentensi.
- Vishazi tegemezi: Kishazi
huru ni kishazi kinachotawaliwa ka kitenzi kisaidizi, ambacho muundo wake
hukifanya kutegemea kitenzi cha kishazi huru ili kuweza kutoa ujumbe
uliokusudiwa. Kishazi tegemezi peke yake hakitoi ujumbe unaojitosheleza
Sifa za Kishazi tegemezi
- Kishazi tegegemezi hutoa maana kamili kinapoandamana na
kishazi huru.
- Kishazi tegemezi kinaweza kufutwa katika sentensi bila
kuharibu maana ya sentensi nzima.
- Kishazi tegemezi hutambulishwa na viambishi vya
utegemezi
- Vinavyoambatanishwa kwenye kitenzi.
- Kishazi tegemezi vile vile kinaweza kutambuliwa kwa
kuwepo vishazi kama vile ingawa, kwamba, ili, kwa sababu, mzizi wa
amba, mofu ya masharti n.k
Aina
ya vishazi tegemezi
Vishazi tegemezi vivumishi
- Vishazi tegemezi vinavyotokea pamoja na nomino
inayovumishwa.
- Vishazi tegemezi visivyoambatana na nomino
inayovumishwa
Vishazi tegemezi vielezi
- Vishazi tegemezi vya mahali
- Vishazi tegemezi vya wakati
- Vishazi tegemezi vya namna au jinsi
- Vishazi tegemezi vya masharti
- Vishazi tegemezi vya hali, hitilafu au kasoro iliyoko
katika tendo.
- Vishazi tegemezi vya sababu/chanzo
Dhima
na hadhi ya vishazi
Kishazi chaweza kuwa huru
kikajitegemea chenyewe kwa kuwa na maana kamili inayojitosheleza. Lakini kuna
vishazi ambavyo havijitoshelezi vyenyewe, bali hutegemea vishazi vingine.
Kishazi huru kina hadhi ya sentensi (sahili). Kishazi tegemezi hakina hadhi
hii, vishazi tegemezi ambavyo hutegemea vishazi vingine hushuka daraja na
kuchukua dhima ya kikundi. Baadhi ya vishazi tegemezi huchukua dhima (hufanya
kazi) ya kivumishi katika tungo ambayo kwa kawaida ni dhima ya kikundi au neno.
Vishazi hivi huvumisha nomino katika tungo hiyo.
Ufafanuzi wa Aina za Tungo
Sentensi
Sentensi ni kifungu cha maneno
kuanzia neno moja na kuendelea chenye muundo wa kiima na kiarifu na kinacholeta
maana kamili.
Sifa za sentensi
Sentensi lazima iwe na mpangilio wa
maneno ambao unakubalika na wazungumzaji wa lugha husika.
- Sentensi lazima ikamilike kimaana, kimuundo na
kisarufi.
- Sentensi huwa na muundo wa kiima na kiarifu /huwa na
kirai nomino na kirai kitenzi.
- Sentensi huweza kuwa na zaidi ya kiima kimoja na
kiarifu zaidi ya kimoja.
- Sentensi inaweza kuundwa na kitenzi kikuu kimoja au
zaidi.
- Sentensi inaweza kuundwa na kishazi huru kimoja au zaidi
na kishazi tegemezi kimoja au zaidi.
- Sentensi huonyesha hali mbalimbali, kama vile amri,
ombi, mshangao, swali n.k
Muundo
wa sentensi
Muundo wa sentensi
kimapokeo/kikazi/kidhima
Muundo wa sentensi
kimapokeo/kikazi/kidhima unakuwa na vipengele vifuatavyo:
- Kiima: Ni
sehemu katika sentensi ambayo hujaza sehemu ya mtenda au mtendwa wa jambo
linaloelezwa. Katika tungo kiima hutokea kushoto mwa kitenzi.
- Kiarifu: Ni
sehemu katika sentensi inayojazwa na maneno yanayo arifu tendo lilofanywa,
linapofanywa au litakapofanywa. Kiarifu ndiyo sehemu muhimu zaidi katika
sentensi ambayo wakati mwengine huweza kusimama pekee, kwani wakati
mwingine huchukua viwakilishi vya kiima.
Vipashio vya kiima
- Nomino peke yake
- Nomino, kiunganishi na nomino
- Nomino na kivumishi
- Kivumishi na nomino
- Kiwakilishi peke yake
- Kiwakilishi na kivumishi
- Nomino na kishazi tegemezi vumishi
- Kitenzi jina
- Nomino na vivumishi zaidi ya kimoja
- Kitenzi jina na nomino
- Umbo kapa
Taarifa zitolewazo na kiarifu kuhusu
kiima
- Kiima ni nani
- Kiima kina nini
- Kiima hufanya nini
- Kiima kinahisi nini
Sifa za kiarifu
- Huwa na kitenzi na pengine huambatana na maneno
mengine.
- Kiarifu kwa kawaida huja baada ya kiima
Vipashio vya kiarifu
- Kitenzi kikuu peke yake.
- Kitenzi kisaidizi au vitenzi visaidizi vilivyosambamba
na kitenzi kikuu.
- Kitenzi kishirikishi na kijalizo
- Yambwa (shamirisho)
- Kijazalio
- Chagizo
Sifa za chagizo
- Chagizo kwa kawaida huwa ni kielezi au kirai husishi
ambacho kinafanya kazi kama kielezi.
- Kwa kawaida ni vipashio vya ziada. Si lazima viwepo
katika sentensi ili ijisimamie.
- Huwa cha lazima ikiwa kinafuata kitenzi kishiriki. Hali
ikiwa hivyo, kinafnaya kazi kama kijalizo.
- Hutumika kufafanua kitenzi/kivumishi /kielezi.
- Hutumika kujaliza kiima/kama kijalizo.
Aina za sentensi
Aina za sentensi kimuundo ni pamoja
na hzi zifuatazo
Sentensi
sahili
Ni sentensi ambayo huundwa na
kishazi huru kimoja. Sentensi ya aina hii huwa inaelezea taarifa moja tu.
Mfano; Wanafuzi wanafanya mtihani; Walinzi walitaka kunizuia nisiingie
ndani.
Miundo ya sentensi sahili
- Muundo wa kitenzi kikuu peke yake. Mfano: Gari
limeanguka
- Muundo wa kitenzi kikuu na kitenzi kisaidizi. Mfano: Mgosiyuda
alitaka (TS) nisipate (T) utajiri
- Muundo wa vira-vitenzi vilivyokitwa katika kitenzi
‘kuwa’. Mfano: John amekuwa akiangalia TV kwa muda mrefu sana.
- Muundo wa kitenzi shirikishi. Mfano: Kiswahili ni tunu
ya Taifa
Sifa za sentensi sahili
- Ina kiima ambacho kimetajwa wazi au kimeachwa kutajwa
kwa kuwa kinaeleweka.
- Ina kiarifu ambacho kimeundwa na kitenzi kikuu kimoja
au kitenzi kikuu na kitenzi kisaidizi au kitenzi kishirikishi na kijalizo
na chagizo.
- Haifungamani na sentensi nyingine na hivi
inajitosheleza kimuundo na kimaana.
Sentensi
changamano
Hii ni sentensi yenye kishazi huru
kimoja au zaidi na kishazi tegemezi kimoja au zaidi. Sifa moja kubwa ya
sentensi changamano ni kuwa na kishazi tegemezi ambacho hutegemea kishazi
kingine huru ndani ya sentensi hiyo. Msingi muhimu wa uhusiano ndani ya
sentensi hizo ni ule wa kishazi kimoja kutegemea kingine
Sentensi changamano ina muundo wenye
vishazi virejeshi. Mfano: Gari liliopinduka jana jioni halikuharibika hatata
kidogo.
Sentensi
ambatano
Hii ni sentensi inayojengwa na
sentensi mbili au zaidi zilizounganishwa kwa kutumia viunganishi kama vile
likini, wala, au, na, nakadhalika.
Miundo ya sentensi ambatano
- Miundo yenye sentensi sahili tu. Mfano: Mwalimu
anafundisha wakati wanafunzi wanapiga kelele.
- Miundo yenye sentensi sahili na changamano. Mfano:
Walinzi waliposhindwa polisi waliwasaidia lakini hawakuweza kuwakamata
majambazi.
- Miundo yenye sentensi changamano tu. Mfano: Barabara
zilizojengwa na wakoloni zimedumu hadi leo wakati zile zilizojengwa na
Wachina hata mwezi hazifikishi.
- Miundo yenye vishazi visivyounganishwa kwa viunganishi.
Uchanganuzi
wa sentensi
Uchanganuzi wa sentensi ni mchakoto
unaohusika na kuchanganua vipashio vyote vinavyuonda sentensi kuanzia ngazi ya
kategoria ya neno. Katika kipengele hiki utaweza kujifunza hatua muhimu za
kuzingatia wakati wa uchanganuzi wa sentensi. Pia utajifunza njia mbalimbali
zinazotumika katika uchanganuzi wa sentensi.
Hatua za uchanganuzi wa sentensi
- Kutaja aina ya sentensi, yaani kama ni sahili,
changamano au ambatano.
- Kutaja sehemu zake kuu, yaani kiima na kiarifu au kirai
nomino na kirai kitenzi.
- Kutaja sehemu kuu za kiima na kiarifu au sehemu kuu za
kirai nomino na kirai kitenzi.
- Kutaja sehemu zote za maneno yaliyomo katika sentensi
hiyo.
Njia za uchanganuzi wa sentensi
Njia ya mishale/mistari
Mfano
Uchanganuzi wa sentensi kwa njia ya
mishale
Njia ya visanduku/jedwali
Mfano
S.S
|
||||||
KN
|
KT
|
|||||
N
|
KH
|
T
|
KN
|
|||
H
|
KN
|
N
|
KV
|
|||
N
|
V
|
KE
|
||||
E
|
||||||
Mtu
|
Mwenye
|
Ulemavu
|
anacheza
|
mpira
|
mzuri
|
sana
|
Njia ya matawi
Mfano
Uchaganuzi wa sentensi kwa njia ya
matawi
Mifano mingine ya uchanganuzi wa
sentensi ambatano; (Watu wengi walimuamini sana lakini yeye aliwasaliti)
Njia ya jedwali
Mfano
Watu wengi walimuamini sana lakini
yeye aliwasaliti
S.A
|
||||||
S1
|
U
|
S2
|
||||
KN
|
KT
|
KN
|
KT
|
|||
N
|
KV
|
T
|
KE
|
W
|
T
|
|
V
|
E
|
|||||
Watu
|
wengi
|
walimwamini
|
Sana
|
Lakini
|
Yeye
|
aliwasaliti
|
Kwa njia ya matawi
Mfano
Watu wengi walimuamini sana lakini yeye
aliwasaliti
Kwa njia ya mishale
Mfano
Watu wengi walimuamini sana lakini
yeye aliwasaliti
MADA YA TATU: MAENDELEO
YA KISWAHILI
Asili ya Kiswahili
Ushahidi
wa Kimsamiati na Kimuundo unaothibitisha Ubantu wa Kiswahili
Neno asili ni jinsi kitu au jambo
lilivyotokea au lilivyoanza. Kutokana na fasili hii tunaona kwamba jambo au
kitu kinaweza kutokea kibahati kama ilivyo katika lugha au linaweza kuanzishwa.
Hivyo basi asili ya lugha ya
Kiswahili bado ni mjadala mrefu ambapo wataalamu mbalimbali wanahitilafiana juu
ya asili au chimbuko la lugha ya kiswahili. Wapo wanaokinasibisha kiswahili na
kiarabu kwa kutumia kigezo cha msamiati na dini ya kiislamu. Wengine
wanashikilia msimamo kuwa kiswahili ni kibantu kwa kutumia hoja za kiisimu na
kihistoria. Wapo wanaokinasibisha kiswahili na uchotara baadhi yao
wanaoshikilia msimamo huu ni Freeman Grenville na Homo Sasson
Kuna nadharia mbalimbali
zinazojaribu kuelezea asili ya Kiswahili, miongoni mwa hizo ni pamoja na hizi
zifuatazo:
Kiswahili
ni Kiarabu
Hapa Kiswahili kimefasiliwa kuwa
asili yake ni kiarabu, wanaoshikilia mtazamo huu wanahoji kwamba katika lugha
ya Kiswahili kuna maneno mengi ya Kiarabu. Pia wanaeleza kuwa asili ya
Kiswahili ni pwani na kwa kuwa wenyeji wa pwani ni Waislamu na kwa kuwa uislamu
uliletwa na Waarabu basi hii lugha ya pwani nayo itakuwa imeletwa na Waarabu.
Vigezo hivyo vyote vina udhaifu mkubwa kwa sababu havikukitwa katika misingi ya
kitaalamu ya uainishaji lugha.
Kiswahili
ni lugha Chotara
Mtazamo huu umezua ubishi mkubwa
kwani hata baadhi ya wazawa wamejinasibisha na uarabu na ushirazi. Wanaofasili
Kiswahili kama lugha chotara wanadai kuwa Kiswahili kimetokana na mchanganyiko
wa lugha ya Kiarabu na lugha za Kibantu. Hivyo Waswahili ni watu waliotokana na
wanaume wa Kiarabu na wanawake wa Kibantu.
Kiswahili
ni lugha ya Vizalia
Waumini wa mtazamo huu wanadai kuwa
Kiswahili kilianza kama pijini ya Kiarabu na baadae kukomaa na kuwa kreoli.
Pijini ni lugha ambayo imetokana na mchanganyiko wa lugha mbili tofauti yaani
Kiarabu na lugha za Kibantu. Na kreoli ni lugha inayozungumzwa na watoto
waliozaliwa na baba Mwarabu na mama Mbantu.
Kiswahili
ni Kikongo
Nadharia hii inafafanua kuwa lugha
ya Kiswahili ilianzia huko Kongo na kusambaa katika pwani ya Afika Mashariki.
Wabatu walipofika Afrika Mashariki waliingia kwa makundi na katika nyakati
mbalibali. Makundi hayo yalianza kujigawa na kutawanyika, matokeo ya
kugawanyika huko ni kutokea kwa makundi mbalimbali ya wabantu. Inasadikika kuwa
baadhi ya Wabantu walifanya maskani yao ya kudumu katika mabonde ya kaskazini
mwa mto tana. Kikundi hiki cha wabantu ndicho inasadikiwa kuwa chimbuko la
Kiswahili
Kiswahili
ni Kibantu
Mtazamo huu ni ule unaoamini kuwa
Kiswahili ni lugha ya Kibantu ambapo lugha za Kibantu zilikuwepo hata kabla ya
majilio ya wageni kutoka Ajemi, Arabuni, India, China na kwingineko. Katika
mtazamo huu lugha ya Kiswahili inaingizwa katika kundi la lugha za Kibantu. Ama
kwa hakika mtazamo huu ulipata mashiko sana kuanzia karne ya ishirini,
ulishadidiwa kutokana na tafiti mbalimbali zilizofanywa na weledi wa isimu,
historia, akiolojia na ethnografia. Wanaisimu waliothibitisha kuwa Kiswahili ni
lugha ya Kibantu ni pamoja na Bleek (1862), Meinholf. C (1932), Malcom Guthrie
(1967, 1970, 1971), Doke (1935, 1945) na wengineo. Vigezo vilivyotumika
kufafanua kuwa Kiswahili ni kibantu ni pamoja na:
- Msamiati
- Mofolojia
- Mfumo wa sauti
- Mfumo wa toni
- Mfumo wa ngeli
- Mpangilio wa maneno
Ubantu wa Kiswahili: Kigezo cha
Kiisimu
Kigezo hiki cha kiisimu kimetumiwa
na wataalam mbalimbali katika kuonesha ubantu wa Kiswahili Massamba (1999)
amewataja wataalam mbalimbali ambao wamehusika na utafiti juu ya ubantu wa
Kiswahili, wataalam hao ni pamoja na Carl Meinhof katika kitabu chake chaIntroduction
to the phonology of the Bantu language,Duke (1935 – 1945), Malcom Guthrie
(1967), Dereck Nurse na Thomas Spear (1985). Hawa walijadili ubantu wa
Kiswahili kwa kutumia kigezo cha kiisimu, kihistoria na kiakiolojia.
Katikakigezo cha kiisimu vipengele
vinavyoangaliwa ni kama vile kufanana kwa msamiati wa msingi, muundo wa
kifonolojia, muundo wa kimofolojia, muundo wa kisintaksia mpangilio wa ngeli za
majina.
Mizizi ya msamiati wa msingiwa lugha za kibantu na Kiswahili hufanana kwa kiasi kikubwa,
mifano ifuatayo huweza kuonesha ukweli huu.
Mfano
Kiswahili
|
Kikurya
|
Kinyiha
|
Kijita
|
Maji
|
Amanche
|
Aminzi
|
Amanji
|
Jicho
|
Iriso
|
Iryinso
|
Eliso
|
Katika mifano hiyo hapo juu tunaona
kuwa mizizi maji, manche, minzi, manji inafanana kwa kiasi kikubwa, kwa hiyo
huu ni ushahidi tosha kutuonesha kuwa kuna uhusiano wa kinasaba kati ya
Kiswahili na lugha za kibantu.
Piamofolojia ya Kiswahili na
lugha za kibantuhufanana kwa kiasi kikubwa, yaani mfumo wa maumbo ya maneno
ya lugha ya Kiswahili na lugha za kibatu hufanana. Kwa mfano, namna viambishi
vinavyopachikwa katika mzizi wa maneno hufuata kanuni ileile kama inavyotumika
katika lugha ya Kiswahili yaani viambishi vinaweza kupachikwa kabla au baada ya
mzizi na huwa na uamilifu bayana.
Mfano
Hebu tuchunguze mifano ifuatayo:
Kiswahili
|
Kisukuma
|
Kisimbiti
|
Kinyiha
|
A-na-lim-a
|
a-le-lem-a
|
a-ra-rem-a
|
i-nku-lim-a
|
a-na-chek-a
|
A-le-sek-a
|
a-ra-sek-a
|
a-ku-sek-a
|
Kwa kuangalia mifano hii utagundua
kwamba katika kutenganisha viambishi hufuata kanuni moja kwamba mahali
kinapokaa kiambishi kwa mfano cha njeo, ndipo pia hukaa kwa upande wa lugha za
kibantu, kwa mfano –na- na –ra- katika lugha ya kisimbiti. Hivyo tunaweza
kusema kuwa kuna unasaba baina ya lugha hizi
Vilevilesintaksiaya lugha ya
Kiswahili na lugha za kibantu hufanana kwa karibu sana. Kwa mfano jinsi yampangilio
wa vipashio na kuunda sentensihufanana yaani mpangilio wa maneno hufuata
kanuni maalum ambazo hufanana katika Kiswahili na lugha za kibantu. Katika
Kiswahili sentesi inakuwa na pande mbili yaani upande wa kiima na upande wa
kiarifu, katika upande wa kiima kipashio chake kikuu ni nomino na katika upande
wa kiarifu kipashio chake kikuu ni kitenzi. Hii inamaana kwamba katika kuunda
sentensi ni lazima nomino ianze na baadaye kitenzi.
Mfano
Hebu tuangalie mifano ifuatayo:
Kiswahili
|
Mama / anakulaN (K) T (A)
|
Kijita
|
Mai / kalyaN(K) T (A)
|
Kihehe
|
Mama/ ilyaN(K) T(A)
|
Kihaya
|
Mama / nalyaN(K) T(A)
|
Katika mifano hii tumeona kwamba
muunndo wa kiima-kiarifu katika lugha za kibantu unafanana sana na ule wa
Kiswahili yaani nomino hukaa upande wa kiima halikadhalika kitenzi hukaa upande
wa kiarifu, kwa hiyo kwa mifano hii tunaweza kusema kuwa lugha ya Kiswahili ni
jamii ya lugha za kibantu.
Piamfumo wa sauti (fonolojia)wa
lugha za kibantu unafana sana na ule wa Kiswahili, yaani mpangilio wa sauti
katika kuunda silabi, na miundo ya silabi kwa ujumla hufanana. Kwa mfano katika
lugha ya Kiswahili hakuna muundo wa silabi funge yaani silabi ambayo inaishia
na konsonanti, muundo asilia wa silabi za Kiswahili ni ule unaoishia na irabu
vilevile katika lugha za kibantu hufuata muundo wa silabi wazi, yaani silabi
zote huishia na irabu.
Mfano
Mifano ifuatayo hufafanua zaidi:
Kisawhili
|
Baba
|
K+I+K+I
|
Kikurya
|
Tata
|
K+I+K+I
|
Kiha
|
Data
|
K+I+K+I
|
Kijita
|
Rata
|
K+I+K+I
|
Kipare
|
Vava
|
K+I+K+I
|
Tanbihi: K= konsonanti I= irabu.
Kwa mifano hii tunaona kwamba mifumo
ya sauti katika lugha za kibantu hufanana na ule wa Kiswahili, kwa hiyo tunaweza
kuhitimisha kwa kusema kuwa lugha hizi ni za familia moja.
Pia vilevilemfumo wa ngeli za
majinakatika lugha ya Kiswahili hufanana sana na ule wa kibantu hususani
katika upachikaji wa maumbo ya umoja na wingi na maumbo ya upatanisho wa
kisarufi. Katika lugha ya Kiswahili viambishi vya umoja na wingi hupachikwa
mwanzoni kabla ya mzizi wa neno, hivyohivyo katika lugha za kibantu
Kwa mfano:
Umoja
|
Wingi
|
|
Kiswahili
|
m-tu
|
wa-tu
|
Kikurya
|
mo-nto
|
abha-nto
|
Kiha
|
umu-ntu
|
abha-ntu
|
Kikwaya
|
mu-nu
|
abha-nu
|
Mifano hiyo hapo juu inadhihirisha
wazi kwamba vipashio vyote vya umoja na wingi hujitokeza kabla ya mzizi wa
neno, hivyo ni dhahiri lugha hizi zina uhusiano wa nasaba moja.
Vilevile katikaupatanisho wa
kisarufilugha za kibantu na Kiswahili huelekea kufanana viambishi vya
upatanisho wa kisarufi hususani viambishi vya nafsi.
Mfano wa viambishi vya nafsi
Kiswahili
|
Mtotoa-nalia
|
Kizanaki
|
Umwanaa-rarira
|
Kisukuma
|
Ng’wanaa-lelela
|
Kikurya
|
Omonaa-rakura
|
Tunaona hapo juu kwamba kiambishi
‘a’ cha upatanisho wa kisarufi hujitokeza katika lugha zote, hivyo
tunashawishika kusema kuwa Kiswahili kina uhusiano mkubwa na kibantu.
Pamoja na ushahidi wa kiisimu
kutupatia vithibitisho tosha juu ya ubantu wa Kiswahili pia kuna ushahidi
mwingine kama vile ushahidi wa kihistoria, kiakiolojia na kiethinolojia.
Ushahidi
wa Kihistoria
Ushahidi wa kihistoria huchunguza
masimulizi na vitabu mbalimbali vya kale ambavyo huelezea asili na chimbuko la
wakazi wa upwa wa Afrika Mashariki. Vilevile ugunduzi wa kiakiolojia huonesha
kuwa kulikuwa na wakazi wa asili wa upwa wa Afrika Mashariki ambao walikuwa na
utamaduni wao na maendeleo yao hata kabla ya kuja kwa wageni. Katika ushahidi
wa kiethinolojia, huchunguzwa tarihi mbalimbali zinazojaribu kutoa historia ya
watu wa pwani ya Afrika Mashariki na lugha yao.
Kwa ujumla vyanzo hivi vyote
huonesha kuwa pwani ya Afrika mashariki ilikuwa na wakazi wake wa asili ambao
walikuwa na lugha yao, utamaduni wao na pia maendeleo yao, vyanzo hivi pia
huhitimisha kwa kusema kuwa lugha ya wakazi hawa ilikuwa ni Kiswahili.
Jinsi Miundo ya Kiswahili
inavyofanana na Miundo ya Lugha nyingine za Kibantu
Fafanua jinsi miundo ya Kiswahili
inavyofanana na miundo ya lugha nyingine za Kibantu
Miundo ya lugha ya za kibantu
inafanana na lugha ya Kiswahili na kufanana huko hutokea katika miundo silabi
ambapo zote huishia na irabu na siyo konsonanti, miundo ya sentensi, miundo ya
vitenzi vya Kiswahili ni sawa na ile ya Kibantu. Kwa mfano vitenzi vya
Kiswahili na kibantu vina uhusiano mkubwa hasa katika viambishi, mnyumbaliko na
pamoja na mianzo na miisho ya vitenzi. Mada hii imefafanuliwa vizuri katika
mada iliyotangulia hapo juu.
Kukua na kuenea kwa Kiswahili nchini Tanzania
katika enzi ya Waarabu
Katika karne ya kumi na tisa Afrika
Mashariki iliingia kwenye mahusiano na mataifa mengine kama vile Marekani,
Ujerumani na Uingereza. Mahusiano haya ni baada ya watu wa pwani kuwa na
uhusiano wa muda mrefu wa kibiashara na Waaarabu, hawa waliweka athari kubwa
katika kukua na kuenea kwa lugha ya Kiswahili. Wageni kutoka Ulaya walipoingia
Afrika Mashariki walifanya biashara, shughuli za kidini (mishenari), elimu na
utawala. Kama ilivyokuwa katika kipindi cha Waarabu, uwepo wao pia ulikuwa na
athari katika maendeleo ya lugha ya Kiswahili Afrika Mashariki na kwingineko.
Ukuaji
wa Kiswahili Kimsamiati nchini Tanzania katika Enzi ya Waarabu
Waarabu hasa katika pwani ya Afrika
Mashariki walifanya biashara ikiwemo biashara ya watumwa. Ilikuwepo misafara
mbalimbali ya biashara kutoka pwani hadi bara. Katika misafara hiyo Kiswahili
ndio ilikuwa lugha ya mawasiliano hivyo Kiswahili kikaenea pia katika sehemu za
bara.
Kuna mambo kadhaa waliyofanya
waarabu ambayo yalichangia kukua kwa lugha ya Kiswahili. Waarabu walichangia
kukua kwa lugha ya Kiswahili kama ifuatavyo:
Biashara
Waarabu walifanya biashara kati ya
pwani na sehemu za bara, katika biashara yao walichangia kwa kiasi kikubwa
uenezaji wa lugha ya Kiswahili. Lugha kuu ya mawasiliano na ya kibiashara
iliyotumiwa na wafanya biashara wa kiarabu ilikuwa ni Kiswahili, kwa hiyo kwa
njia hii waliweza kueneza Kiswahili kuanzia pwani hadi maeneo ya bara kama vile
Tabora, Kigoma hadi mashariki mwa Kongo.
Dini
Dini pia ni jambo ambalo liliweza
kuchangia ueneaji wa lugha ya Kiswahili enzi za waarabu. Waarabu walipokuja
walitaka kueneza dini yao kwa undani kabisa. Kwa hivyo iliwabidi kuanzisha
madarasa ambayo walitumia kufundishia, lugha iliyokuwa ikitumiwa ni lugha ya
Kiswahili. Na hivyo hii ikasaidia kuenea kwa lugha ya Kiswahili.
Maandishi ya kiarabu
Waarabu pia walileta hati zao
zilizotumiwa katika maandishi ya lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo kupitia hati za
kiarabu maandishi mbalimbali ya lugha ya Kiswahili yaliweza kuhifadhiwa, hivyo
Kiswahili kiliweza kukua kwa vile kingeweza kuhifadhiwa katika maandishi na
kusomwa wakati wowote.
Kuoana
Pia vilevile Waarabu waliofika pwani
waliweza kuoana na wabantu, hii ilisababisha kizazi kipya kutokea. Na kwa
sababu hiyo watoto walichukua maneno mengi kutoka kwa baba na mama yao na hivyo
kuongeza msamiati katika lugha Kiswahili.
Ueneaji
wa Kiswahili nchini Tanzania katika Enzi ya Waarabu
Waarabu walieneza Kiswahili nchini
Tanzania kupitia biashara, kuoana na wabantu au wenyeji wa pwani, kupitia dini
na maandishi ya hati za kiarabu ambayo yalitumika kuhifadhi maandishi
mbalimbali ya lugha ya Kiswahili.
Kukua na kuenea kwa Kiswahili nchini Tanzania
katika enzi ya Wajerumani
Wajerumani waliingia katika pwani ya
Afrika Mashariki katika miaka ya 1875, walifanya kila jitihada kuwatawala Waafrika
ambapo katika utawala wao walifanya biashara, waliendesha shughuli za
kiutawala, za kidini na kielimu. Katika shuguli zote hizo Kiswahili ndio
ilikuwa lugha ya mawasilino hivyo kukikuza na kukiendeleza Kiswahili
Walipongia katika pwani ya Afrika Mashariki
walikuta Kiswahili kimekwisha enea kwa kiasi kikubwa. Kuna mambo waliyoyafanya
ambayo yalisaidia kukua na kuenea kwa Kiswahili kama ifuatavyo:
Kutoa
mafunzo ya lazima ya lugha ya Kiswahili kwa wafanyakazi wa serikali
Waliwalazimisha wafaanyikazi wote wa
serikali kujifunza kiswashili, kwa sababu sheria ilikuwa ni kwamba pasipojua
Kiswahili huwezijiriwa katika serekali ya mjerumani. Kwa hiyo saula hili
lilisababisha watu kujifunza lugha ya Kiswahili ili waweze kuajiriwa.
Wafanyakazi ambao ilikuwa ni lazima wajifuze Kiswahili ni pamona na maakida.
Wajerumani wenyewe walilazimika
kujifunza kiswahili ili waweze kuwasiliana na wenyeji kwa urahisi na hivyo
kurahisisha shuguli zao za kiutawala.
Ujenzi
wa shule
Shule zilifunguliwa kufundisha watu
weusi ili waje wawe wasidizi wao katika utawala wa wajerumani, na lugha
iliyokuwa ikitumika kufundisha masomo ilikuwa ni lugha ya Kiswahili
Kuenea kwa utawala wa Wajerumani
nchi nzima
Utawala wa wajerumani ulikuwa kwenye
kila kona ya nchi. Na kwa kuwa wafanya kazi wa serikali ya wakati huo ilikuwa
ni lazima wafahamu Kiswahili, kwa hiyo kila sehemu palipokuwa na ofisi za
serikali nchi nzima kulizungumzwa Kiswahili.
Shughuli
za kiuchumi
Pia katika shuguli za mashamba,
wajerumani walichukua vibarua kutoka sehemu mbalimbali za nchi, na kwa kuwa
kila mmoja alikuwa na lugha yake tofauti, kwa hiyo lugha pekee iliyowaunganisha
katika mawasiliano kwenye eneo la kazi ilikuwa ni Kiswahili.
Kwa hiyo kutokana na sababu kwamba
utawala wa kijerumani ulitoa msukumo mkubwa katika matumizi ya lugha ya
Kiswahili kwenye shughuli zao za kiutawala, hivyo suala la ueneaji wa Kiswahili
lisingeepukika.
Ueneaji wa Kiswahili nchini Tanzania katika
Enzi za Wajerumani
Wajerumani walichangia kwa sehemu
kubwa kuenea kwa lugha ya Kiswahili nchini Tanzania enzi za utawala wao. Mambo
yaliyochangia kuenea kwa lugha ya Kiswahili enzi za utawala wa Wajerumani ni
pamoja na dini, elimu, shughuli za utawala na shughuli za kiuchumi kama vile
kilimo.
MADA YA NNE: UHAKIKI WA KAZI ZA
FASIHI ANDISHI
Fasihi andishi ni tawi la fasihi
linalotumia sanaa ya maneno kufikisha ujumbe kwa hadhira kwa njia ya maandishi.
Zipo aina nyingi za fasihi andishi, miongoni mwa hizo ni pamoja na hadithi
fupi, riwaya, tamthiliya na mashairi.
Maana ya Uhakiki
Dhana ya Uhakiki
Uhakiki ni kitendo cha kutathimini,
kueleza, kuainisha na kutoa maoni juu ya kazi fulani ya fasihi kwa kuongozwa na
kaida maalum. Hii ina maana kwamba uhakiki wa kazi za fasihi hautoki katika
ombwe, kuna kanuni na taratibu mbalimbali zinazoongoza kufanya uhakiki, na hii
ndio sababu kuna nadharia kadha wa kadha za uhakiki wa kazi za kifaishi. AU kwa
lugha rahisi tunaweza kusema, uhakiki ni uchambuzi wa kina wa kazi za fasihi
kama vile riwaya, tamthiliya na mashairi kwa lengo la kufafanua vipengele vya
fani na maudhui.
Misingi
ya Uhakiki
Kwa ujumla mhakiki wa kazi za fasihi
anapofanya uhakiki wa kazi za kifasihi, huwa analenga vipengele viwili. Pengine
analenga kuhakikifaniya kazi husika aumaudhuiya kazi hiyo na
wakati mwingine vyote viwili. Kwa hiyo kupitia vipengele hivi ndipo atachambua
vitu vingi kama vile ujumbe, falsafa, matumizi ya lugha, dhamira, mandhari na
kadhalika.
Kuhakiki Fani
Katika utunzi wa kazi za kifasihi,
Fani hutumika kama nyezo ya kuwasilisha mawazo ya mwandishi kwa njia ya kisanaa
zaidi. Fani ni mbinu anayoitumia mwandshi ili kufikisha ujumbe kwa watu
aliowakusudia.
Vipengele vya fani ni pamoja nawahusika,
mandhari, lugha, muundo na mtindo.
Mtindo
Mtindo ni mbinu ya kipekee kifani na
kimaudhui, zinazotofautisha msanii mmoja na mwingine. Kwa mfano, namna msanii
anavyotumia lugha, anavyoteua msamiati, namna anavyosimulia hadithi yake
(anaweza kutumia nafsi ya kwanza, ya pili au ya tatu). Kwa mfano katika riwaya
ya “Barua Ndefu kama hii” iliyoandikwa na Mariama Ba ametumia mtindo wa barua
ya kirafiki kuanzia mwanzo hadi mwisho, hii pia inaonesha mtindo wake wa
kipekee.
Muundo
Muundo ni mpangilio wa kiufundi
anaoutumia mwandishi katika kupangilia kazi yake. mpangilio na mtiririko wa
kazi ya fasihi, kwa upande wa visa na mtukio.
Kuna aina mbili za kupangilia
matukio
- Msago; hii ni namana ya moja kwa moja ya kusimulia
matukio, yaani kuanzia tukio la kwanza hadi la mwisho kwa namna
yalivyotukia. Huu ni muundo wa moja kwa moja.
- Urejeshi; huu ni usimuliaji wa kurukaruka hatua, yaani
msimuliaji anaweza kuanzia katikati, akaja mwisho na kumalizia na mwanzo
Wahusika
Wahusika; ni watu au viumbe ambavyo
mwandishi wa fasihi huwatumia ili kufanikisha ujumbe kwa jamii husika. Katika
kazi ya fasihi mwandishi huwagawa wahusika katika makundi mawili yaani wahusika
wakuu na wahusika wadogo.
Wahusika wakuu ni wale ambao
wanajitokeza kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa kazi ya fasihi. Wahusika wadogo ni
wale wote ambao wanajitokeza sehemu mbalimbali katika kazi ya fasihi kwa mfano,
mwanzoni mwa kitabu hadi mwishoni mwa kitabu.
Wahusika hawa wawe ni wakuu au
wadogo wanaweza kugawanyika katika makundi yafuatayo:
- Mhusika mviringo
ni mhusika ambaye anabadilika kitabia na kimawazo kulingana na hali halisi
ya maisha. Kwa mfano wanaweza kuanza kama watu wema lakini hali ya maisha
ikawabadilisha na kuwa watu wabaya au wanaweza kuanza kama watu wabaya na
hali ya maisha ikawabadilisha na kuwa watu wema.
- Mhusika bapa
ni mhusika ambaye habadiliki kulingana na hali halisi ya maisha. Mfano;
kama ni mwema basi atakuwa mwema kuanzia mwanzo wa hadithi hadi mwisho na
kama ni mbaya basi atakuwa mbaya kuanzia mwanzo wa hadithi hadi mwisho.
- Mhusika shinda
yuko katikikati ya mhusika papa na mviringo. Huongozwa na matendo ya hao
wahusika wawili. Hajitokezi na msimamo wake imara.
Mandhari
Mandhari; hii ni sehemu ambayo
matukio ya hadithi au masimulizi hutokea. Mandhari huweza kuwa halisi kama vile
baharini, njiani, msituni, kijijini, mijini au ya kufikirika kama vile kuzimu,
mbinguni, peponi n.k.
Lugha
Lugha ndio nyenzo kubwa ya msanii
katika kazi za fasihi, miongoni mwa vipengele vya lugha ni tamathali za semi
pamoja na semi.
Fani za Lugha
- Tanakali za Sauti: Ni
mbinu ya kutumia maneno yanayoiga sauti au hali fulani au namna kitendo
kilivyofanyika.
- Tashbiha:
Hii ni mbinu ya lugha inayolinganisha vitu au hali mbili tofauti kwa
kutumia maneno ya kulinganisha; ‘kama’, ‘mithili ya’, ‘sawa na’, ‘ja’.
mfano, Mwembamba kama sindano.
- Tashihisi:
Hii ni mbinu ya kupatia kitu kisicho hai sifa za kiumbe mwenye uhai (sifa
za kibinadamu). Mfano, "Sungura aliposhindwa, akasema sizitaki hizi
mbichi".
- Takriri:
Ni mbinu ya kurudiarudia neno moja au kifungu cha maneno ili kusisitiza
ujumbe fulani. Mfano, alikimbia, alikimbia, alikimbia hadi akashika nafasi
ya kwanza.
- Ukinzani:
Ukinzani ni mbinu ya kusisitiza ujumbe kwa kuambatanisha maneno ya kinyume
au yanayokinzana.
- Sitiari:
Ni mbinu ya kulinganisha vitu viwili moja kwa moja kwa kutumia kiungo ‘ni’
ama ‘kuwa’. Mfano; Maisha ni mlima, juma ni mwamba.
- Taswira:
Ni matumizi ya lugha/maneno yanayojenga picha ya hali au jambo fulani kwa
msomaji.
- Taashira:
Ni matumizi ya lugha ya ishara kuwakilisha ujumbe fulani. Jina au kitu
fulani kinatumika kumaanisha kitu kingine chenye uhusiano na kile
kilichotumiwa.
- Jazanda:
Ni kulinganisha vitu viwili moja kwa moja bila kutumia viunganishi.
- Majazi:
Majazi ni pale tabia za wahusika zinapoambatana na majina yao halisi.
- Lakabu:
Ni mbinu ya mhusika kupewa/kubandikwa jina na wahusika wengine ama yeye
mwenyewe kujibandika jina linalooana na tabia/sifa zake.
- Chuku:
Ni kutumia maneno yaliyotiliwa chumvi ili kusisitiza ujumbe fulani au
kusifia kitu, kutilia Chumvi.
Semi
Ni fungu la maneno linapotumika
kutoa maana nyingine, badala ya ile ya maneno yaliyotumika. Semi hutumika
kuficha ukali wa maneno au kupamba lugha. Kuna aina mbili za semi:
- Nahau – ni usemi unaotumia maneno ya kawaida kwa lengo
la kufikisha maana iliyotofauti na maana ya kawaida ya maneno hayo. Nahau
huwa na vitenzi.
- Misemo – ni semi fupifupi ambazo hutumiwa mara kwa mara
kwa lengo la kuleta maana maalumu. Misemo haina vitenzi.
- Maswali ya Balagha:
Tashititi au maswali ya balagha ni maswali yanayoulizwa na msimulizi au
mhusika ambayo hayahitaji jibu.
- Uzungumzi Nafsiya:
Mhusika hujizungumzia, ama kwa kuongea au kuwaza, bila kukusudia kusikika
na yeyote.
- Ritifaa:
Mbinu ya kuzungumza na mtu aliyekufa (au asiyekuwepo) kana kwamba yuko
pamoja nawe.
- Kuchanganya Ndimi: Kuweka maneno yasiyo ya
Kiswahili katika sentensi ya Kiswahili. Mfano, "alisimama kwanza kwa
muda, before he went aliniambia nisimwambie mtu yeyote yule, you
know!"
- Kuhamisha Ndimi:
Ni kuingiza sentensi ya lugha nyingine katika kifungu cha lugha ya
Kiswahili. Kinyume na Kuchanganya ndimi (ambapo mwandishi huchanganya
maneno katika sentensi moja, katika kuhamisha ndimi, sentensi kamilifu ya
lugha nyingine hutumika miongoni mwa sentensi za Kiswahili sanifu. Mfano:
Kazi hii ni ngumu sana, sitaweza kuifanya. People are trying to convince
me to stay here but I think I can't, I must go!
- Mathali:
Methali ni misemo ya hekima yenye maana iliyofumbwa. Mhusika, mwandishi wa
fasihi anaweza kutumia methali kupitisha ujumbe.
Mbinu nyingine za Kisanaa
- Kinaya:
Kinaya ni mambo katika sanaa kuwa kinyume na matarajio ya hadhira.
- Kejeli;
Kejeli ni mbinu ya sanaa inayotumia maneno kudharau au kukemea kitendo au
mtu fulani.
- Taharuki;
Taharuki ni mbinu ya kusimulia au kuandika riwaya/hadithi kwa kufanya
hadhira na/au wahusika wajawe na hamu ya kutaka kujua kitakachotokea
baadaye; hamu ya kutaka kuendelea kusoma/kusikiliza. Baadhi ya hadithi
huishia kwa taharuki na kuilazimisha hadhira yake ijikamilishie au ibaki
ikijiuliza maswali.
- Sadfa;
Sadfa ni kugongana kwa vitendo viwili vinavyohusiana kana kwamba vilikuwa
vimepangwa, japo havikuwa vimepangiwa.
- Kisengere Nyuma;
Mwandishi ‘hurudi nyuma’ na kuanza kusimulia kisa kilichokuwa kimetendeka
kabla ya alichokuwa akisimulia. Aidha, mwandishi hubadilisha wakati wa
masimulizi na kuwa wakati wa kisa hicho. Hutumika sana kuonyesha mhusika
anapokumbuka kitu, au kutupatia msingi wa jinsi mambo yalivyoanza.
- Kisengere Mbele;
Mwandishi anapobadilisha wakati na kusimulia mambo yatakavyokuwa siku za
usoni; au kutumia lugha isiyo moja kwa moja kutabiri yatakayojiri.
Utabiri.
Kuhakiki Maudhui
Maudhui; Maudhui katika kazi ya
fasihi ni jumla ya mawazo yote yanayozungumzwa pamoja na mtazamo wa mwandishi
juu ya mawazo hayo. Maudhui hujumuisha mawazo pamoja na mafunzo mbalimbali
yaliyomsukuma msanii hadi akatunga na kusanii kazi fulani ya kifasihi.
Vipengele vya maudhui ni pamoja na dhamira, migogoro, falsafa ujumbe na
msimamo.
- Dhamira;
hili ni wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika kazi ya
fasihi. Dhamira ni sehemu tu ya maudhui na aghalabu dhamira kuu ndio
hujenga kiini cha kazi ya fasihi. Dhamira zimegawanyika katika makundi
mawili, kuna dhamira kuu na dhamira ndogondogo.
- Migogoro;
hii ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi za fasihi. Migogoro
inaweza kuwa kati ya wahusika, familia zao, matabaka yao, au hata katika
nyadhifa mbalimbali. Vilevile migogoro yaweza kuwa ya kiuchumi, kijamii,
mogogoro ya nafsi, na migogoro ya kisiasa ambayo hujitokeza katika
mitazamo tofauti kulingana na mtiririko wa visa na matukio yanavyopangwa
na mwandishi.
- Ujumbe;
mwandishi anapoandika kazi yake huwa na ujumbe ambao hutaka uifikie jamii
aliyoikusudia. Ujumbe katika kazi fasihi ni mafunzo mbalimbali ambayo
hupatikana baada ya kusoma kazi ya fasihi. Katika kazi ya fasihi dhamira
kuu hubeba ujumbe wa msingi na dhamira ndogondogo hubeba ujumbe ambao
husaidia kuujenga au kuupa uzito zaidi ujumbe wa msingi.
- Msimamo;
katika kazi ya fasihi, mawazo, mafunzo na falsafa ya msanii hubainisha
msimamo wake kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii. Msimamo ni ile hali ya
mwandishi kuamua kufuata na kushikilia jambo fulani. Jambo hili huweza
kukataliwa na wengi lakini akalishikilia tu. Msimamo ndio huweza
kuwatofautisha wasanii wawili au zaidi wanaoandika kuhusu mazingira
yanayofanana. Kwa mfano, katika tamthilia ya “Pesa zako zinanuka”
mwandishi anamsimamo wa kimapinduzi kwani amejadili matatizo yanayochangia
kukwama kwa ujenzi wa jamii mpya.
- Falsafa
ni mawazo ya busara yenye kutawaliwa na misingi mahususi juu ya asili na
maana ya ulimwengu na maisha ya mwanadamu. Ni msimamo wa msanii katika
maisha juu ya utatuzi wa matatizo katika jamii. Falsafa ya mwandishi
inaweza kujulikana kwa kusoma kazi zake zaidi ya moja.
- Mtazamo
ni hisia au uelewa wa mwandishi juu ya jambo fulani. Kwa mfano anaweza
kutazama jambo fulani kwa mtazamo wa kidini, au anaweza kutazama jambo
fulani kwa mtazamo wa kisiasa au kisayansi.
- Mafunzo;
ni mawazo ya kuelimisha yanayopatikana katika dhamira mbalimbali za kazi
ya fasihi.
Kufaulu na Kutofaulu kwa mwandishi
Kufaulu au kutofaulu kwa mwandishi
kunategemea jinsi alivyoweka uwiano mzuri kati ya fani na maudhui kwa namna
ambavyo inaleta uhalisia. Mfano, endapo msanii atakuwa na mhusika Mkongo lakini
akawa anazungumza kiswahili kilichojaa misemo na nahau alafu kimenyooka kama
mtu wa pwani itakuwa vigumu kusema amefaulu kwani hakuna uwiano mzuri kati ya
mhusika mwenyewe na lugha anayoitumia. Kiswahili cha Kongo ni tofauti kabisa na
kiswahili kinachozungumzwa na watu wa pwani (Tanzania).
Uhakiki wa Fani katika Kazi za Fasihi Andishi
Uhakiki wa Fani katika Tamthiliya
Uhakiki wa fani katika Ushairi
Uhakiki wa Maudhui katika Kazi za Fasihi Andishi
Uhakiki wa Maudhui katika Tamthiliya
Uhakiki wa Maudhui katika Ushairi
MADA YA TANO: UTUNGAJI WA KAZI
ZA FASIHI ANDISHI
Utungaji wa Hadithi
Mikondo ya Hadithi
Kazi za fasihi andishi ni sanaa,
yaani zinahitaji ubunifu wa mwandishi ili ziwe katika mwonekanao huo wa
kisanaa. Fasihi andishi hutumia lugha na wala sio lugha tu bali lugha ya
kisanaa, kama tulivyokwishaona katika mada zilizotangulia kwamba lugha ni
kipengele muhimu sana katika fasihi. Ili kazi ya kifasihi ya msanii husika iwe
nzuri na ya kuvutia, masanii hana budi kuwa na ubunifu wa hali ya juu katika
kutumia lugha.
Msanii awe na uwezo wa kupangilia
maneno, kuteua maneno katika hali ya ujumi lakini pia yakiwa yamebeba ujumbe
unaoigusa hadhira yake. Kwa maana hii mwandshi wa kazi za kifasihi, iwe riwaya
au tamthilia ni lazima azingatie sana lugha, kwani lugha ndio nyenzo kuu ya
usanaa wa fasihi kwa ujumla.
Kuna hatua kadhaa za kuzingatia
wakati wa kuandika kazi ya kisanaa, hatua hizo ni kama zifuatazo:
- Kuwa na kisa/wazo unalotaka kuliandikia: Katika jamii kuna mambo mengi sana yanayotendeka,
msanii anaweza kupata wazo la kiubunifu kutokana na mambo hayo
yanayotendeka katika jamii. Kama tujuavyo fasihi andishi kazi yake ni
kuonesha yale yanayotendeka katika jamii, kwa hiyo msanii anaweza kutumia
fursa hiyo ili kuweka wazi mambo yanayoendelea katika jamii. Kwa mfano
mwandishi naweza kutunga kazi ya kibunifu kuhusu, ufisadi, umasikini,
mapenzi, ndoa, maisha yake mwenyewe, ushirikina, jambo lolote analoliamini
katika maisha (falsafa yake). Kwa hiyo hatua ya kwanza kwa msanii kabala
ya kuandika ni kuelewa vizuri jambo analotaka kuandikia. Pia katika hatua
hii msanii anaweza kubuni jina la hadithi yake, pia hii inaweza kumsaidia
katika upangaji wa visa na matukio ya hadithi yake.
- Kuchagua umbo la kazi ya fasihi: Msanii akishapata wazo la kuandika, sasa inambidi
achague jinsi atakavyoliwasilisha wazo lake hilo. Yaani anaweza kuchagua
endapo aandike hadithi fupi, riwaya au tamthiliya, au ushairi au utenzi.
Sasa uchaguzi wa umbo la kazi ya fasihi unategemeana na uwezo wa msanii
katika tanzu hizo, kuna mwingine anapenda tamthiliya lakini kuandika
riwaya hawezi, kuna mwingine anaona kuandika ushairi ni rahisi na kuna
mwingine hawezi. Kwa hiyo ubunifu wa msanii utadhihirika katika utanzu ule
anaoumudu vizuri zaidi.
- Kubaini hadhira:
Mwandishi kujua yule anayemwandikia ni suala la msingi sana. Hadhira ipo
ya watu wa aina mbalimbali, watoto, watu wazima, wasomi, wenye elimu
ndogo, wakulima, wanasiasa n.k. Sasa mwandishi akishabaini hadhira
anayoindikia itamsaidia kuteua lugha ya kuandikia, kwa mfano kama ni
watoto, hatutegemei mwandishi kutumia lugha ngumu, misemo na nahau nyingi.
- Kubuni wahusika na mandhari: Mwandshi baada ya kujua kazi yake inahusu nini sasa
inambidi abuni wahusika wa hadithi yake. Wahusika wanaweza kuwa ni watu,
wanyama, mimea, mazimwi, malaika n.k. Pia ni lazima abaini mazingira
ambamo visa vyote vya hadithi na matukio yatakapofanyika. Mandhari
yanaweza kuwa baharini, kijijini, mjini, mbinguni, kuzimu n.k
- Kupanga msuko wa visa na matukio: Msuko wa visa na matukio ni muhimu sana katika
usimulizi wa hadithi. Sasa kama mwandishi amaeamua kuwasilisha kazi yake
kwa njia ama ya hadithi fupi au riwaya au tamthiliya ni vema ajue namna
visa na matukio vitakavyopangwa. Katika kufanya hivi maswali yafuatayo ni
muongozo mzuri katika kupangilia ploti: Hadithi yangu itaanzaje? Mgogoro
utaanzaje? Ni kati ya nani na nani? Je, kilele cha mgogoro ni nini? Je, ni
mhusika mkuu kubakwa na kuambukizwa VVU? Hadithi yangu inaishaje? Je
mhusika mkuu ashindwe? Atorokee nje ya nchi? Afungwe? Abadilike Au maadui
ndio wafungwe au wafe? Au wabadilike?
- Kuanza kuandika:
Sasa baada ya kupitia hatua hizo zote, mwandishi sasa anaweza kuanza
kuandika. Mchakato wa kuandika hua ni mrefu na mwandishi anaweza kujikuta
anafuta mara nyingi kile alichokiandika, hii ni kutokana na kwamba mambo
mengi ya kuandika huwa yanakuja wakati mwandishi ameanza kuandika kazi
husika. Hata hvyo sio vibaya kufanya hivi, hii pia inasaidi kuwa na zao
bora la fasihi.
Utungaji wa hadithi
Hadithi ni masimulizi ya kubuni
yaliyoandikwa kinathari inaweza kuwa na wahusika wengi, matukio mengi na
mandhari mapana (inategemena na aina ya hadithi, iwapo ni hadithi fupi wahusika
wake huwa ni wachache na pia matukio ni machache, mandhari yake pia ni finyu).
Kuna aina zifuatazo za hadithi kulingana na kigezo cha urefu au maudhui. Kwa
kigezo cha urefu kuna Hadithi Fupi na Riwaya. Kutokana na maudhui
kuna Riwaya Dhati na Riwaya Pendwa.
Riwaya dhati ni zile zinazozungumzia
masuala muhimu ya kijamii, kama vile uonevu wa tabaka la chini, rushwa, uongozi
mbovu n.k
Riwaya pendwa ni hadithi zenye lengo
la kuburudisha, kutokana na usimuliaji wake uliojaa taharuki na fantasia. Mambo
yanayosimuliwa katika riwaya hizi ni yale yanayogusa hisia za watu kwa urahisi
kama vile mapenzi, mauaji, ujasusi n.k.
Mikondo ya uandishi wa hadithi
Mkondo wa hadithi ni mwelekeo ambao
mwandishi anaufuata katika utunzi wa kazi yake. Mikondo ya utunzi wa hadithi ni
pamoja na hii ifuatayo:
- Mkondo wa kiwasifu;
mkondo huu huhusisha hadithi zote zinazosimulia maisha ya watu. Ni riwaya
ambayo inasimulia maisha ya mtu toka alipozaliwa hadi wakati huo.
- Mkondo wa kitawasifu;
hadithi zinazofuata mkundo huu ni zile zinazosimulia maisha ya mtu binafsi
yaani mwandishi mwenyewe. Kwa mfano riwaya ya “maisha yangu baada ya Miaka
hamsini”. (S.Robert)
- Mkondo wa kihistoria;
hadithi katika mkondo huu zinahusu matukio ya kweli ya kihistoria
yaliyotokea. Kwa mfano riwaya ya “Uhuru wa Watumwa”
- Mkondo wa kipelelezi;
hizi ni hadithi zinazozungumzia upelelezi wa uhalifu fulani kama vile
ujambazi, wizi, rushwa, mauaji n.k.
- Mkondo wa kimapenzi;
katika mkondo huu zinaingia riwaya zote zinazozungumzia masuala ya
mapenzi.
Utungaji
wa hadithi fupi
Kama tulivyokwisha ona hapo nyuma
sifa za hadithi fupi, basi katika utungaji wake mambo yafuatayo ni sharti
yazingatiwe:
- Hadithi fupi inakuwa na mhusika mkuu mmoja ambaye
anajitokeza sana kuliko wahusika wengine.
- Idadi ya wahusika ni ndogo ukilinganisha na wahusika wa
kwenye riwaya.
- Mandhari ya hadithi fupi si mapana kama ilivyo katika
riwaya
- Hadithi fupi inakuwa inaongelea dhamira kuu moja tu
ambayo inaonekana toka mwanzo hadi mwisho wa hadithi.
Utungaji Wa Kazi Za Fasihi Andishi
Utungaji wa Hadithi
Mikondo ya Hadithi
Kazi za fasihi andishi ni sanaa,
yaani zinahitaji ubunifu wa mwandishi ili ziwe katika mwonekanao huo wa
kisanaa. Fasihi andishi hutumia lugha na wala sio lugha tu bali lugha ya
kisanaa, kama tulivyokwishaona katika mada zilizotangulia kwamba lugha ni
kipengele muhimu sana katika fasihi. Ili kazi ya kifasihi ya msanii husika iwe
nzuri na ya kuvutia, masanii hana budi kuwa na ubunifu wa hali ya juu katika
kutumia lugha.
Msanii awe na uwezo wa kupangilia
maneno, kuteua maneno katika hali ya ujumi lakini pia yakiwa yamebeba ujumbe
unaoigusa hadhira yake. Kwa maana hii mwandshi wa kazi za kifasihi, iwe riwaya
au tamthilia ni lazima azingatie sana lugha, kwani lugha ndio nyenzo kuu ya
usanaa wa fasihi kwa ujumla.
Kuna hatua kadhaa za kuzingatia
wakati wa kuandika kazi ya kisanaa, hatua hizo ni kama zifuatazo:
- Kuwa na kisa/wazo unalotaka kuliandikia: Katika jamii kuna mambo mengi sana yanayotendeka,
msanii anaweza kupata wazo la kiubunifu kutokana na mambo hayo
yanayotendeka katika jamii. Kama tujuavyo fasihi andishi kazi yake ni
kuonesha yale yanayotendeka katika jamii, kwa hiyo msanii anaweza kutumia
fursa hiyo ili kuweka wazi mambo yanayoendelea katika jamii. Kwa mfano
mwandishi naweza kutunga kazi ya kibunifu kuhusu, ufisadi, umasikini,
mapenzi, ndoa, maisha yake mwenyewe, ushirikina, jambo lolote analoliamini
katika maisha (falsafa yake). Kwa hiyo hatua ya kwanza kwa msanii kabala
ya kuandika ni kuelewa vizuri jambo analotaka kuandikia. Pia katika hatua
hii msanii anaweza kubuni jina la hadithi yake, pia hii inaweza kumsaidia
katika upangaji wa visa na matukio ya hadithi yake.
- Kuchagua umbo la kazi ya fasihi: Msanii akishapata wazo la kuandika, sasa inambidi
achague jinsi atakavyoliwasilisha wazo lake hilo. Yaani anaweza kuchagua
endapo aandike hadithi fupi, riwaya au tamthiliya, au ushairi au utenzi.
Sasa uchaguzi wa umbo la kazi ya fasihi unategemeana na uwezo wa msanii
katika tanzu hizo, kuna mwingine anapenda tamthiliya lakini kuandika
riwaya hawezi, kuna mwingine anaona kuandika ushairi ni rahisi na kuna
mwingine hawezi. Kwa hiyo ubunifu wa msanii utadhihirika katika utanzu ule
anaoumudu vizuri zaidi.
- Kubaini hadhira:
Mwandishi kujua yule anayemwandikia ni suala la msingi sana. Hadhira ipo
ya watu wa aina mbalimbali, watoto, watu wazima, wasomi, wenye elimu
ndogo, wakulima, wanasiasa n.k. Sasa mwandishi akishabaini hadhira
anayoindikia itamsaidia kuteua lugha ya kuandikia, kwa mfano kama ni
watoto, hatutegemei mwandishi kutumia lugha ngumu, misemo na nahau nyingi.
- Kubuni wahusika na mandhari: Mwandshi baada ya kujua kazi yake inahusu nini sasa
inambidi abuni wahusika wa hadithi yake. Wahusika wanaweza kuwa ni watu,
wanyama, mimea, mazimwi, malaika n.k. Pia ni lazima abaini mazingira
ambamo visa vyote vya hadithi na matukio yatakapofanyika. Mandhari
yanaweza kuwa baharini, kijijini, mjini, mbinguni, kuzimu n.k
- Kupanga msuko wa visa na matukio: Msuko wa visa na matukio ni muhimu sana katika
usimulizi wa hadithi. Sasa kama mwandishi amaeamua kuwasilisha kazi yake
kwa njia ama ya hadithi fupi au riwaya au tamthiliya ni vema ajue namna
visa na matukio vitakavyopangwa. Katika kufanya hivi maswali yafuatayo ni
muongozo mzuri katika kupangilia ploti: Hadithi yangu itaanzaje? Mgogoro
utaanzaje? Ni kati ya nani na nani? Je, kilele cha mgogoro ni nini? Je, ni
mhusika mkuu kubakwa na kuambukizwa VVU? Hadithi yangu inaishaje? Je
mhusika mkuu ashindwe? Atorokee nje ya nchi? Afungwe? Abadilike Au maadui
ndio wafungwe au wafe? Au wabadilike?
- Kuanza kuandika:
Sasa baada ya kupitia hatua hizo zote, mwandishi sasa anaweza kuanza
kuandika. Mchakato wa kuandika hua ni mrefu na mwandishi anaweza kujikuta
anafuta mara nyingi kile alichokiandika, hii ni kutokana na kwamba mambo
mengi ya kuandika huwa yanakuja wakati mwandishi ameanza kuandika kazi
husika. Hata hvyo sio vibaya kufanya hivi, hii pia inasaidi kuwa na zao
bora la fasihi.
Utungaji wa hadithi
Hadithi ni masimulizi ya kubuni
yaliyoandikwa kinathari inaweza kuwa na wahusika wengi, matukio mengi na
mandhari mapana (inategemena na aina ya hadithi, iwapo ni hadithi fupi wahusika
wake huwa ni wachache na pia matukio ni machache, mandhari yake pia ni finyu).
Kuna aina zifuatazo za hadithi kulingana na kigezo cha urefu au maudhui. Kwa
kigezo cha urefu kuna Hadithi Fupi na Riwaya. Kutokana na maudhui
kuna Riwaya Dhati na Riwaya Pendwa.
Riwaya dhati ni zile zinazozungumzia
masuala muhimu ya kijamii, kama vile uonevu wa tabaka la chini, rushwa, uongozi
mbovu n.k
Riwaya pendwa ni hadithi zenye lengo
la kuburudisha, kutokana na usimuliaji wake uliojaa taharuki na fantasia. Mambo
yanayosimuliwa katika riwaya hizi ni yale yanayogusa hisia za watu kwa urahisi
kama vile mapenzi, mauaji, ujasusi n.k.
Mikondo ya uandishi wa hadithi
Mkondo wa hadithi ni mwelekeo ambao
mwandishi anaufuata katika utunzi wa kazi yake. Mikondo ya utunzi wa hadithi ni
pamoja na hii ifuatayo:
- Mkondo wa kiwasifu;
mkondo huu huhusisha hadithi zote zinazosimulia maisha ya watu. Ni riwaya
ambayo inasimulia maisha ya mtu toka alipozaliwa hadi wakati huo.
- Mkondo wa kitawasifu;
hadithi zinazofuata mkundo huu ni zile zinazosimulia maisha ya mtu binafsi
yaani mwandishi mwenyewe. Kwa mfano riwaya ya “maisha yangu baada ya Miaka
hamsini”. (S.Robert)
- Mkondo wa kihistoria;
hadithi katika mkondo huu zinahusu matukio ya kweli ya kihistoria
yaliyotokea. Kwa mfano riwaya ya “Uhuru wa Watumwa”
- Mkondo wa kipelelezi;
hizi ni hadithi zinazozungumzia upelelezi wa uhalifu fulani kama vile
ujambazi, wizi, rushwa, mauaji n.k.
- Mkondo wa kimapenzi;
katika mkondo huu zinaingia riwaya zote zinazozungumzia masuala ya
mapenzi.
Utungaji wa hadithi fupi
Kama tulivyokwisha ona hapo nyuma
sifa za hadithi fupi, basi katika utungaji wake mambo yafuatayo ni sharti
yazingatiwe:
- Hadithi fupi inakuwa na mhusika mkuu mmoja ambaye
anajitokeza sana kuliko wahusika wengine.
- Idadi ya wahusika ni ndogo ukilinganisha na wahusika wa
kwenye riwaya.
- Mandhari ya hadithi fupi si mapana kama ilivyo katika
riwaya
- Hadithi fupi inakuwa inaongelea dhamira kuu moja tu
ambayo inaonekana toka mwanzo hadi mwisho wa hadithi.
MADA YA SITA: ANDISHI WA INSHA
NA MATANGAZO
Uandishi wa Insha za Kisanaa
Misingi ya Kuandika Insha
Insha za kisanaa ni insha
zinazoelezea mambo ya kawaida katika jamii lakini kwa kutumia lugha ya kisanaa.
Lugha ya kisanaa ni pamoja na matumizi ya tamathali za semi, misemo nahau,
methali na taswira.
Muundo
wa Insha
Kwa kawaida insha inakuwa na sehemu
kuu nne: kichwa cha insha, utangulizi, kiini na hitimisho.
- Kichwa cha insha; Kichwa
cha insha hudokeza kile utachokijadili katika insha yako, hubainisha wazo
kuu la mada inayohusika. Kwa kawaida kichwa cha insha huandikwa kwa
sentensi fupi. Mfano; maisha ya kijijini, mimba za utotoni.
- Utangulizi; Mambo
yaliyopo katika utangulizi ni pamoja na kutoa fasili ya maneno muhimu na
kuelezea kwa muhtasari mambo ambayo utakwenda kuyajadili katika insha
yako. Utangulizi unakuwa katika aya moja fupi.
- Kiini cha insha;
Katika kiini ndipo kuna maelezo ya kina juu ya kile unachokijadili katika
insha yako, maelezo haya yanakuwa katika aya kadhaa kulingana na idadi ya
hoja ulizonazo katika mjadala wako.
- Hitimisho;
Hapa ndipo kuna muhtasari wa kile kilichojadiliwa katika kiini cha insha
au inaweza kuwa ni msimamo juu ya kile kilichojadiliwa katika insha.
Insha za Kisanaa
Insha ya kisanaa ni ile inayotumia
lugha ya kisanaa yaani yenye tamathali za semi kama vile sitiari, tashbiha,
taniaba na mubalagha. Aidha insha ya kisanaa hutumia mbinu nyingine za kisanaa
kama tashititi, takriri, na tanakali sauti. Vilevile insha za kisanaa huwa na
lugha zenye mvuto na misemo kama nahau, methali na tamathali za semi.
Uandishi wa Matangazo
Tangazo ni taarifa za wazi zinazotoa
ujumbe fulani kwa walengwa wanaohusika na ujumbe huo. Ujumbe unaweza kuwa na
lengo la kushawishi, kuarifu, kuelekeza, na kadhalika.
Vipengele vya Kuzingatiwa katika
Uandishi wa Mtangazo
Malengo ya matangazo
- Kutoa taarifa;Lengo
mojawapo la matangazo ni kutoa taarifa, mfano wa matangazo yanayotoa
taarifa ni mialiko, tangazo la kifo, alama za barabarani, matangazo ya
kazi.
- Kuonya;
Matangazo pia yana lengo la kuonya, kwa mfano matangazo kama vile ya
kutovuta sigara, UKIMWI na kadhalika.
- Kushawishi;
Matangazo pia yana lengo la kushawishi, matangazo yenye lengo hili mara
nyingi ni matangazo ya biashara ambayo kwa kweli lengo lake ni kushawishi
wateja ili wanunue bidhaa zao, mtangazo ya mialiko hasahasa ya tukio
fulani, labda msanii anazindua albamu fulani na kadhalika.
Jinsi ya kuandika matangazo
Ili tangazo liweze kufanikisha
kufikia lengo lililokusudiwa kuna mambo kadhaa ya kufanya; mambo hayo ni kama
yafuatayo:
- Kichwa cha habari;
Mara nyingi matangazo yanakuwa na kichwa cha habari, hii inasaidia kujua
kwa haraka kuwa tangazo linahusika na kitu gani.
- Kuonesha aina ya bidhaa/huduma; Hiki ndicho kiini cha tangazo, hapa tangazo linaonesha
ujumbe uliokusudiwa kufikishwa kwa wahusika, sasa ujumbe huu waweza kuwa
ni bidhaa inayotangazwa au huduma inayotolewa au kazi inayotangazwa au
mwaliko unahusu nini.
- Anwani;
Hapa tangazo linaonesha mahali ambapo watoa tangazo walipo, yaani ofisi
zao zilipo ambapo wahusika wa tangazo wanaweza kwenda na kuwakuta. Kama ni
tangazo la mwaliko basi ni lazima lionesha shughuli yenyewe itafanyika
wapi.
- Njia za mawasiliano;
Kama ni tangazo la biashara au la kazi au la mwaliko ni muhimu kutoa
mawasiliano. Mawasiliano hayo yanaweza kuwa ni namba ya simu, fax, wavuti
(kwa taarifa zaidi), barua pepe.
Mbinu za uandishi wa matangazo
Ili tangazo liweze kuvuta umakini wa
watu ni lazima liwe na mwonekanao fulani. Zifuatazo ni mbinu za uandishi wa
matangazo.
- Matumizi ya picha; Matangazo
mengi ya biashara huwa yanaambatana na picha, picha hizi hujaribu
kumshawishi mteja aamini kuwa ile bidhaa ni bora na hivyo ni muhimu kuwa
nayo au kuinunua.
- Maneno machache;
Matangazo hutumia maneno machache kwa lengo la kutomchosha mlengwa lakini
wakati huohuo maneno hayo yana nguvu ya kumshawishi mlengwa.
- Lugha ya kisanii;
Maneno ya kisanii katika matangazo huwa ni mepesi kukumbukwa na huwa
yanaeleweka kirahisi. Kwa mfano, matumizi ya vivumishi, litakuwa ni bonge
la shoo, njoo ujinunulie pamba za ukweli, n.k. Matumizi ya
mubalagha, kwa mfano; mtandao unaoongoza Tanzania, mganga bingwa afrika
mashariki na kati n.k
- Matumizi ya watu maarufu; Matangazo mengi hususani ya biashara hupenda kutumia
watu maarufu ili kuwashawishi walengwa. Kwa mfano kama ni tangazo juu ya
bidhaa fulani, huweza kumwonesha pengine msanii maarufu, miss Tanzania, au
mchezajia mpira maarufu. Sasa mlengwa anapoona kwamba hata mtu maarufu
anatumia hiyo bidhaa, anashawishika na yeye kuitumia
MADA YA SABA:
KUSOMA KWA UFAHAMU
Kusoma Kimya
Ufahamu wa kusoma ni ule mtu
anaoupata kwa njia ya kusoma makala, kifungu cha habari, kitabu au gazeti.
Maswali ya Ufahamu kutokana na
Habari uliyosoma
Katika ufahamu wa kusoma, msomaji
anatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo:
- Kubaini mawazo makuu;
msomaji anaposoma habari fulani au kitabu inatkiwa ajiluze, Je,
kinachoongelewa hapa nini? Ni jambo gani hasa analolizungumzia mwandishi?
Msomaji akiwa na maswali haya akilini mwake basi itakuwa rahisi kwake
kuielewa habari hiyo.
- Kuzingatia alama za uakifishi; msomaji ni lazima azingatie alama za uakifishi, kwa
kufanya hivyo itamsaidia kuelewa ujumbe wa habari hiyo na endapo
hatazingatia alama za uakifishaji anaweza kupotosha maana ya mwandishi.
- Kubaini maana ya maneno na misemo mbalimbali; habari nyingine huwa zina maneno ya kisanaa hivyo ni
muhimu msomaji kubaini maana ya maneno hayo katika muktadha wa habari
hiyo, hii itamsaidia kuelewa vyema maana ya mwandishi.
- Vilevile msomaji anatakiwa kumakinikia kile
anachokisoma, kila kipengele anachokisoma inampasa akielewe vizuri.
Kwa kuzingatia haya yote msomaji atakuwa
na uelewa mzuri juu ya habari aliyoisoma na pia anaweza kufupisha habari hiyo
aliyoisoma
Kufupisha
habari
Kufupisha habari ni kuandika upya
habari uliyoisoma kwa maneno machache lakini bila kupotosha ujumbe wa habari ya
kwanza.
Ufupisho wa habari huwa na sifa
hizi:
- Huwa ni mfupi kuliko habari ya mwanzo
- Huwa na ujumbe uleule uliokuwa katika habari ya mwanzo
- Hujumuisha mawazo makuu yaliyodondolewa kutoka kwenye
habari ya mwanzo
- Mawazo haya sharti yapangwe katika mtririko wenye
mantiki
Hatua za kufuata katika kuandika
ufupisho
Ili kuweza kufanikiwa kufupisha
habari kwa ufanisi hatua zifuatzo sharti zifuatwe:
- Kuisoma au kuisilikiza habari kwa makini ili kuielewa
vizuri
- Kutambua na kubaini mawazo makuu yanayojitokeza katika
kila aya
- Kuyaunganisha mawazo makuu na kuandika au kuelezea
ufupisho wa habari hiyo kwa maneno yako mwenyewe bila kupostosha maana ya
habari ya kwanza.
- Kuhesabu idadi ya maneno ya ufupisho ili kuyapunguza
ikiwa yanazidi idadi iliyotakiwa.
- Kama muda unaruhusu pitia tena habari ya mwanzo na
pitia tena ufupisho ili kujiridhisha kuwa hujaacha taarifa yoyote ya
muhimu.
Kufupisha
Habari Uliyoisoma
Mtu mmoja na mkewe kutoka jamii ya
Daliti inayobaguliwa tangu jadi nchini India wameuawa, mmoja akiwa amekatwa
kichwa na mwengine kunyongwa kwa kushindwa kulipa deni la Rupee kumi na tano
ambalo ni karibu senti ishirini na mbili tu.
Polisi kaskazini mwa taifa hilo
wamethibitisha kisa hicho ambapo yasemekana mfanyi biashara anayetokea jamii ya
hadhi ya juu,aliwaua wanandoa hao kwa kushindwa kulipa deni la biskuti
walizokuwa wamewachukulia watoto wao.
Mfanyi biashara huyo
amekamatwa.Ubaguzi kwa misingi ya kijamii umeenea sana nchini India, huku watu
wa jamii ya Daliti waliokuwa wamebadikwa jina la 'the untouchables' wakiwekwa
kwenye daraja la chini kabisa kwenye sera hiyo ya kibaguzi nchini India iitwayo
'caste' ambapo wananyimwa fursa nyingi za kimaendeleo na hivyo kubaki katika
lindi la umaskini.
Hata hivyo Visa vya ukatili wa
kibaguzi dhidi ya jamii ya Dalit katika jimbo la Gujarat vimeongezeka mnamo siku
za hivi karibuni na vimesababisha wimbi la maandamano kutoka watu wa jamii
hiyo.
Zoezi
Kwa maneno yasiyozidi 30 fupisha
habari uliyoisoma hapo juu.
4 Comments
Well done Mashallah
ReplyDeleteNahitaji nukuu za kiswahili
ReplyDeleteKISWAHILI
ReplyDeleteNaitaji notes za masomo yote
ReplyDelete